SINGIDA UNITED, LIPULI NA NJOMBE FC JIPANGENI MSIISHIE KUSINDIKIZA VPL


Na Dina Ismail
LIGI kuu soka Tanzania bara  inaelekea ukingoni ambapo  mshike mshike upo katika makundi mawili, zile zinazowania ubingwa wa msimu wa 2016/17 na zenye kupambana na kushuka daraja.
Katika mbio za kuwania ubingwa, vigogo vya soka nchini Simba na Yanga ndizo zinazopambana kuwania ubingwa wa ligi hiyo, huku Majimaji, Toto Africans,JKT Ruvu na Mbao Fc zikiwa katika mchuano wa mojawapo kujikwamua kubaki Ligi kuu kwani timu tatu za mwisho zitashuka.
Msimu mpya wa ligi 2017/2018 utazikaribisha timu za Singida United (Singida), Lipuli Fc  na Njombe mji zote kutoka mkoani Iringa ambako timu hizo kwa sasa zimeshaanza maandalizi kwa na namna moja ama nyingine.
Singida United na Lipuli Fc si mara yao ya kwanza kushiriki katika ligi hiyo ambako mara ya mwisho zilishiriki ilikuwa miaka 17 iliyopita na kisha kushuka daraja.
Njombe mji yenyewe yenye maskani yake katika mji wa Njombe mkoani Iringa hii itakuwa mara yake ya kwanza kushiriki katika ligi kuu.
Kwa wanaofuatilia historia ya soka la bongo na hasa Ligi Kuu ni wazi kwamba wanazifahamu sana Singida United na Lipuli na hiyo inatokana na umahiri wao ilizokuwa nazo enzi zinashiriki ligi hiyo.
Tuseme ni bahati mbaya tu kwao ilipelekea kushuka daraja lakini  ni timu ambazo zilikuwa na wachezaji wenye vipaji vya hali ya juu kiasi ambacho vigogo vya soka nchini Simba na Yanga ziliweza kuvuna wachezajaji kutoka huko kwa nyakati tofauti.
Kwa sasa timu hizo zipo katika maandalizi ya msimu mpya wa ligi kuu na ili kuweza kushiriki vyema tayari zimeanza mikakati madhubuti ya kuimarisha vikosi v yake, benchi la ufundi na miundombinu yake, yaani viwanja vya mazoezi.
Timu ya Singida United kwa kuonesha kuwa imejipanga vema kushiriki kikamilifu tayari imefanya maboresho kwenye benchi lake la ufundi kwa kumuajiri aliyepata kuwa kocha na Mkurugenzi wa benchi la Yanga, Hans Van Der Pluijm.
Kama hiyo haitoshi, Singida United pia imeanza usajili wake kwa kuwasajili wachezaji watatu wa  kimataifa kutoka Zimbabwe, Tafadzwa Kutinyu, Elisha Muroiwa   na Wisdom Mtasa.
Singida United pia ipo katika ukarabati wa hali ya juu wa Uwanja wa Namfua ambao itautumia katika ligi hiyo kama uwanja wake wa nyumbani.Zoezi hilo linafanywa na Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Singida.
upandaji wa nyasi huku ikielezwa ifikapo Agosti mechi zote za nyumbani zitachezwa uwanjani hapo.
Singida United ambayo imemwajiri kocha mpya Mholanzi, Hans Pluijm  na kusajili wachezaji watatu wa kigeni ni miongoni mwa timu tatu zilizopanda daraja kushiriki ligi kuu msimu ujao pamoja na Njombe Mji na Lipuli FC.
Kwa upande wa Lipuli Fc, ambayo iko chini ya Chama cha soka Mkoa wa Iringa (IRFA) iliyochukua jukumu la kuiendesha klabu hiyo kutokana na  kuwepo kwa  mgogoro uliozuka ndani ya uongozi wa klabu hiyo,nayo ipo katika mipango ya kujiweka sawa ili kushiriki vema katika ligi hiyo.
Njombe Mji Fc ambayo inanolewa na kocha maarufu nchini, Hassan Banyai nayo imedhamiria kuhakikisha inashindana na si kushiriki kwenye ligi hiyo kubwa nchini.
Kwa mantiki hiyo, timu hizo zitacheza ligi hiyo kiushindani zaidi na si kufanya bora liende na hasa ikizingatia zilifanya juhudi na jitihada kubwa kuhakikisha zinapanda hadi ligi hiyo.
Kwamba, ziwe mfano kwa timu nyingine zinazopanda kwa kufanya vema na hata ikiwezekana mojawapo itwae ubingwa au hata kuingia tatu bora mwishoni mwa ligi.
Ushiriki wao usiwe nguvu za soda kwa kuishia kuzifunga tu Simba na Yanga halafu mechi nyingine zinapoteza, zitakuwa zimewakosea sana wananchi na pia kupoteza nguvu, heshima na jitihada bure za wakazi wa miji ya Iringa na Singida ambao walikuwa nazo bega kwa bega mpka zinapanda.

Aidha, ni vema timu hizo zikajiepusha na siasa za Simba na Yanga, kuanzia katika usajili na hata kipindi watakachoanza kushiriki Ligi Kuu, zicheze soka la ushindani kama zilivyofanya katika Ligi daraja la kwanza.

Comments