TIMU LIGI KUU ZITHAMINI VIJANA WAKE



Na Dina Ismail
SHIRIKISHO la  soka Tanzania (TFF) miaka kadhaa iliyopita liliweka kanuni ya kila timu inayoshiriki ligi Kuu soka Tanzania Bara kuwa na timu za Vijana, yaani ile ya miaka chini  ya 17 na 20.
TFF ilifanya hivyo kwa minajiri ya kuinua na kuendeleza soka la Tanzania, pia kusaidia kupatikana kwa hazina ya wachezaji kwa ajili ya baadaye.
Kama hiyo haitoshi, ilianzisha ligi maalum ya timu hizo za vijana ambayo imekuwa ikifanyika kipindi ambacho mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Bara unakuwa umesimama.
Kwa kiasi kikubwa michuano hiyo imekuwa ikileta na msisimko mkubwa kutokana na wachezaji wa timu husika kuonesha vipaji vya hali ya juu.
Pia kupitia michuano hiyo, kumetoa nafasi kwa viongozi wa timu zao kuona wachezaji ambao wanafaa kupandishwa hadi timu za wakubwa.
Lakini, ukiangalia ama kufuatilia kwa umakini utabaini kwamba baadhi ya timu hizo za vijana ‘zipo zipo’  kwani hata lengo la kuinua na kuendeleza vipaji halitiliwi maana.
Kwamba, timu za vijana zipo lakini kipindi cha usajili viongozi wanahaha kusaka wachezaji toka Simba, Yanga, Azam, Kagera Sugar na kadhalika badala ya kupandisha wachezaji wa timu zao za vijana.
Ni sawa kwao kusaka wachezaji wenye uzoefu, lakini angalau wangekuwa wanachukua hata wachezaji watano kutoka katika kikosi cha cha vijana na kasha nafasi zingine ndio kusaka magwiji na wale wa kigeni.
Kwani bila ya kuwapandisha katika kikosi cha wakubwa itakuwa ni sawa na kuuwa vipaji vyako na kuzidi kudumaza soka la Tanzania.
Kama hiyo haitoshi, kupandisha daraja wachezaji wa timu hizo za vijana kutasaidia kubana matumizi kwa kiasi fulani kwani tumeshuhudia mamilioni ya pesa yakitumika kusajili wachezaji wazoefu na wale ‘mapro’.
Swali la kujiuliza, kuna faida gani ya kuwa na timu za vijana kama hawawezi kupandishwa madaraja, mwisho wa siku inakuwa mchawi wa soka ni timu zenyewe kwani zinashindwa kuvuna matunda yake na kwenda kusaka ya nje.
Angalau tunaona baadhi ya wachezaji waliopandishwa kutoka timu za vijana wakichanua katika timu zao kwa misimu kadhaa lakini baada ya muda wanapotea katika medani ya soka.
Baadhi ya wachezaji kama Frank Domayo , Haruna Chanongo, Ramadhan Singano, Jonas Mkude, Hassan Isihaka, Peter Manyika na wengineo ni baadhi ya matunda ya timu za vijana katika Ligi Kuu Bara.
Kama hiyo haitoshi, majina ya wachezaji hao yalikuwa chaguo la mara kwa mara katika vikosi vya timu ya Taifa kwa nyakati tofauti.
Sijui tatizo ni nini, kwani kwa sasa moto wa nyota hao chipukizi umezimika ghafla na wengi wameachwa katika timu zilizowapandisha, huku wengine wakiishia kukosa namba katika kikosi cha kwanza.
Na kwa hali ilivyo itawawia vigumu sana kurejesha hadhi yao kama ilivyokuwa mwanzo na hiyo inatokana na mfumo wa soka la Tanzania ulivyo.
Tulitaraji viwango vyao vingedumu kwa muda mrefu kama ilivyokuwa enzi za kina Sekilojo Chambua, Madaraka Suleiman, Mohammed Manyika, George Masatu, Mohammed Hussein ‘Mmachinga’ na wengineo, lakini imekuwa tofauti na sasa hivi tunaweza kusema  ‘wapo wapo’.
Thomas Ulimwengu na Mbwana Samatta ni mfano wa kuigwa kwa wachezaji ‘chapuo’ la timu za vijana, kwani hawa wana vipaji pia kama walivyo wenzao lakini wasimamizi wao walisoma alama za nyakati, na leo hii ni ‘habari nyingine’.
Nadhani ni wakati muafaka kwa vilabu vya ligi kuu kuiga wa nchi zilizopiga hatua katika medani ya soka ambazo kuwapa nafasi zaidi wachezaji vijana ambao wakisimamiwa vema wataleta manufaa katika siku za usoni.
Tunaona wachezaji wengi nyota wa Ulaya wameibuka wakiwa wadogo na wamejitahidi kwa kiasi kikubwa ‘kumantain’ viwango vyao kwa muda mrefu na hatimaye ili tuweze kuwa na mafanikio katika soka.
Lakini kwa Tanzania bado hatuwatilii maanani wachezaji chipukizi,na tumekuwa tukikumbatia wachezaji wakongwe tu ambao baadhi yao hawana hata viwango vikubwa kama ilivyo kwa vijana lakini tunaona wakipewa nafasi.
Kwani hata hao waliobahatika kuwemo wameshindwa kulelewa ipasavyo matokeo yake wamejikuta wakiishia katika pasi na kufika safari yao.
Kwa hali hiyo nashindwa kuelewa faida ya kuanzishwa kwa timu B maana uwepo wake ni kama kutimiza wajibu tu!


Comments