IVO MAPUNDA SPORTS CENTER NA DHAMIRA YA KUINUA VIPAJI



Na Dina Ismail

GOLIKIPA  mkongwe wa Tanzania, Ivo Mapunda  wiki  iliyopita alifungua kituo maalum cha kuibua na kuendeleza vipaji  vya  soka kwa vijana wadogo  wenye umri wa kuanzia miaka mitano hadi 18.
Kituo hicho kilichopo maeneo ya Mwanagati, Kitunda huko jijini Dar es Salaam kitajulikana kama Ivo Mapunda Sports Center.
Katika miaka ya hivi  karibuni, kumekuwa na urasimu wa uwepo wa vituo vingi vya namna hiyo   kwani  vingi ‘vipovipo’ tu  kwa vile  wachezaji wengi wazuri ambao wanatamba na kufanya vema katika medani ya soka nchini hawatokei huko.
Nchi zilizoendelea katika soka zina utitiri mwingi wa vituo vya namna hiyo hivyo kuwepo kwa ushindani wa wachezaji ambao wamepitia huko pindi wanapofanikiwa kuanza kucheza soka la ushindani, tofauti na hapa nchini ambapo wachezaji wengi wanaibuka wakutokea  mitaani.
Kwamba matokeo yake  tumekuwa tukitegemea wachezaji wale wale, hali inayofanya soka la Tanzania lizidi kudumaa na matokeo yake kushindwa kufurukuta kwenye medani za  kimataifa.
Ivo Mapunda anasema anaamini ujio wa kituo hicho utasaidia kuleta changamoto katika medani ya soka na hasa ikizingatiwa  amepata kuwamo katika timu mbalimbali hivyo anaamini atazalisha vipaji stahili.
“Nimekuwa  mchezaji ndani na nje ya nchi kwa miaka mingi hivyo kwa uzoefu wangi nitawapa mbinu nzuri za kuwafanya waweze kufika mbali baada ya kumaliza  mafunzo yao katika kituo change,”anasema
Mapunda  ambaye alipata kuzidakia timu kongwe anasema anaongeza kuwa kituo hicho pia “nimeanzisha kituo hiki ili kusaidia vijana wasio na kazi hivyo itasaidia kupata ajira kupitia michezo,”anaongeza
Anasema pamoja na mafunzo ya soka kituo hiko kitakuwa kikiwapa ushauri wa kujitambua vijana hao ili iwe rahisi kwao kukabiliana na changamoto watakazokutana nazo katika safari zao za kucheza soka la kiushindani.
“Ni matumaini yangu vijana watakaotoka hapa watakuwa katika ngazi nyingine, nimedhamiria kuleta mapinduzi katika vituo vya vijana, hivyo ninaomba sapoti ya wazazi na Watanzania kwa ujumla ili tuweze kuzalisha wachezaji wazuri”,anaongeza Mapunda
Ivo Philip Mapunda ni mmoja ya makipa waliojijengea heshima hapa nchini ambaye kwa sasa hachezi soka la ushindani tangu alipoachwa na klabu yake ya Azam mwaka 2015 na hivyo amekuwa akifanya mazoezi mtaani kwa ajili ya kujiweka fiti.

Mapunda ambaye aliwahi kuwemo kwenye kikosi cha timu ya Taifa, pia amepata kuzidakia pia timu za Gor Mahia ya Kenya, St.George ya Ethiopia na Congo United kwa nyakati tofauti.

Comments