SAFARI LAGER YAIPIGA JEKI TIMU YA WAVU YA JWTZ

KAMPUNI ya Bia Tanzania (TBL) kupitia bia yake ya Safari, imejitosa kudhamini Chama cha Darts Tanzania (Tada) katika mashindano ya mchezo huo kwa timu za Jeshi la Wananchi(JWTZ), Polisi na Magereza  ‘Majeshi Challenge Cup’ ambapo pia imedhamini mashindano ya Jeshi la Wananchi pekee yanayotarajiwa kuanza kutimua vumbi Julai 5 hadi 7 mwaka huu katika ukumbi wa Jeshi la Wananchi, Msasani jijini Dar es Salaam.
Meneja wa Bia ya Safari, Oscar Shelukindo alisema mashindano hayo yatakuwa ya kila mwaka kwakuwa wameamua kudhamini mashindano hayo ili kuinua mchezo wa Darts, kuhamasisha na kuburudisha majeshi nchini.
Alisema thamani ya udhamini wa mashindano hayo likiwemo la Jeshi la Wananchi pekee litakalo julikana kama Ngome Darts Challenge ni sh. Milioni 16 na laki mbili ambapo fedha hizo ni kwamichuano yote miwili ikijumuisha zawadi, maandalizi na gharama za kuendesha mashindano.
“TBL kupitia bia ya Safari tumeamua kudhamini mashindano haya ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mipango yetu kuendeleza michezo na kushiriki katika shughuli za kijamii hapa nchini ambapo huu ni mwaka wa tatu mfululizo kwa kampuni yetu kupitia bia ya Safari kudhamini mashindano mbali mbali ya Darts nchini na hata katika ukanda wa Afrika Mashariki” alisema Shelukindo.
Katika Mashindano ya Darts kombe la Majeshi yaliyoanza kutimua vumbi Juni 28 na kuhitimishwa juzi, timu ya Lugalo ilijinyakulia kitita cha sh. 500,000 baada ya kuibuka bingwa wa mashindano hayo huku Polisi Barack wakijinyakulia sh. 300,000 baada ya kukamata nafasi ya pili ambapo washindi wa tatu na nne Polisi Barack A na Ngome Dar es Salaam wakijinyakulia kitita cha sh. 150,000 ambapo washiriki wengine kutoka Polisi Mbeya, na Mzinga wakiondoka na kifuta jasho cha sh. 100,000 pamoja na zawadi za vikombe, fulana, na ndara kwa washiriki wote.

Naye Katibu wa Tada, Kale Mgonja aliwashukuru TBL kupitia bia ya Safari kwa kuweza kufanikisha mashindano hayo ambapo wanaamini mashindano yajayo yatakuwa na ubora zaidi katika kuuendeleza mchezo huo kote nchini.

Comments