YANGA BILA BRANDTS WAANZA KULINOLEA MAKALI KOMBE LA KAGAME

MABINGWA wa soka Tanzania Bara na Afrika Mashariki na Kati, Yanga SC leo wameanza rasmi mazoezi bila ya kocha wake mkuu, Ernie Brandts ambayo ameshindwa kurejea nchini juzi kama ilivyopangwa.
Baadhi ya wachezaji wa Yanga walifanya mazoezi hayo katika Uwanja wa shule ya sekondari ya Loyola, Mabibo, Dar es Salaam chini ya kocha msaidizi Freddy  Felix Minziro. 
Ofisa habari wa Yanga Baraka Kizuguto amesema kwamba karibu wachezaji wote waliopo nchini walihudhuria mazoezi hayo. 
Alisema kocha Brandts ambaye alikuwa kwao kwa ajili ya mapumziko alishindwa kuwasaili nchini juzi anatarajiwa kuwasili wakati wowote na kuendelea na majukumu yake ya kukinoa kikosi hicho. 
Aliongeza kuwa kwa sasa wachezaji hao watakuwa wakifanya mazoezi ya kawaida huku wakiwasubiri wachezaji wengine waliomo katika timu za Taifa ambazo zinajiandaa na mechi za kufuzu fainali za kombe la Dunia zitakazopigwa mwishoni mwa wiki hii. 
Wachezaji wa Yanga waliopo kwenye timu za Taifa ni pamoja na Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Mrisho Ngassa, Ali Mustafa ‘Barthez’ Frank Domayo, Simon Msuva na Athuman Iddi ‘Chuji’ ambao wapo katika kikosi cha Taifa Stars kinachojiandaa kwa ajili ya mchezo wake na Morocco. 
Wengine ni wachezaji wa kimataifa Haruna Niyonzima na Mbuyu Twite waliopo timu ya Taifa ya Rwanda ‘Amavubi’ na Hamis Kiiza aliyepo kikosi cha Uganda ‘The Cranes’. 
Yanga, Simba na Super Falcon ya Zanzibar zitashiriki michuano ya Kagame inayotarajiwa kuanza kutimua vumbi kuanzia Juni 18 hadi Julai 2 huko Sudan Kusini. 

Mabingwa hao watetezi wamepangwa kundi C pamoja na Vital’O ya Burundi, Express ya Uganda  na Ports ya Burundi ambapo wataanza kutetea taji lao juni 20 kwa kucheza na Express.

Comments