WAREMBO 11 kutoka sehemu mbalimbali wamejitokeza kushiriki
shindano la kumsaka malkia wa kitongoji cha Kigamboni mwaka huu "Redd's
Miss Kigamboni 2013" linalotarajiwa kufanyika Ijumaa Juni 7 kwenye ukumbi
wa Navy Beach kuanzia saa 2:00 usiku hapa jijini Dar es Salaam.
Tayari warembo wameshaanza mazoezi kwa ajili ya kujiandaa na
shindano hilo ambapo wanajifua kwenye ukumbi wa Break Point (VIP) uliopo Posta
hapa jijini.
Mratibu wa shindano hilo,
Somoe Ng'itu (pichani), alisema kuwa maandalizi ya shindano hilo yako katika hatua za
mwisho na bado wanakaribisha warembo wenye sifa za kushiriki shindano hilo
kufika mazoezini kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini.
Aliwataja warembo ambao wameshaanza mazoezi kuwa ni pamoja
na Rogathe Michael, Irene Rajab, Magdalena Olotu, Latifa Mohammed, Axsaritha
Vedastus, Angella Lutataza, Sara Makembo, Amina Mussa, Ellen Sulle, Julieth Mwanri na Rachel Reuben.
"Tunatarajia kuwa na shindano lenye mvuto na
litakalotoa washindani kwenye mashindano ya kanda na baadaye katika ngazi ya
taifa, tumejipanga kufanya mapinduzi ndani ya sanaa hii ya urembo wa hapa
nchini," alisema Somoe.
Aliongeza kwamba fomu kwa ajili ya kushiriki shindano hilo
zinapatikana bure na warembo wanafanya mazoezi chini ya Blessing Ngowi, ambaye
mwaka juzi alishiriki fainali za taifa za Redd's Miss Tanzania na alitwaa taji
la Kanda ya Elimu ya Juu.
Aliyataka makampuni na taasisi mbalimbali zinakaribishwa
kudhamini shindano hilo ambalo mwaka jana lilitoa mshindi katika kinyang'anyiro
cha Kanda ya Temeke ambaye ni Edda Sylivester.
Wadhamini ambao wamethibitisha kusaidia shindano hilo ni
pamoja na kampuni ya bia Tanzania kupitia kinywaji cha Redd's Premium Original,
Montage Limited, Clouds Media Group, Papa Z na Break Point.
Taji la Redd's Miss Tanzania linashikiliwa na Brigitte
Alfred wakati Edda alishika alifanikiwa kushika nafasi ya tatu kwenye fainali
hizo za taifa mwaka jana.
Comments
Post a Comment