LICHA YA KUTOA KAZI NZURI ZA WASANII LAKINI MTAYARISHAJI TUDD THOMAS BADO HASHUKURIWI

Prodyuza Tudd Thomas.
MASHABIKI wa mtayarishaji wa muziki (Producer), mwenye uwezo wa kipekee, aliyetayarisha wimbo wa Leka dutigite wa Kigoma All Stars na zingine nyingi, Tudd Thomas, wamekuwa wakiulizana maswali mengi wao kwa wao pasipo kupata majibu.
Safari ya Tudd Thomas katika muziki, ilianzia mkoani Iringa akiwa Iringa Records aliporekodi wimbo wa mwanamuziki Marlaw unaoitwa Bembeleza. Wimbo huo ulipata tuzo ya wimbo bora wa mwaka kutoka Kilimanjaro Tanzania Music Awards mwaka 2008 na pia kumfanya Marlaw apate tuzo ya msanii bora wa kiume kupitia tuzo hizo. Baadae alihamia jijini Dar es Salaam na ndipo alipoonesha uwezo wake zaidi kwa kusuka nyimbo zilizotikisa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla.
Hakuna asiyeufahamu wimbo wa Pii Pii (Missing my baby) wa Marlaw ambao aliutengeneza yeye kupitia Studio ya JML. Wimbo huo ulipata tuzo nyingi ikiwa ni pamoja na tuzo ya Nzumari nchini Kenya mwaka 2009 mbapo uliingia kwenye kipengere cha wimbo bora wa Afrika Mashariki, kumfanya Marlaw aingie kwenye kipengele cha msanii bora wa Afrika Mashariki na kunyakua tuzo hiyo. Baada ya hapo wimbo huo ulipata tuzo ya Kilimanjaro nchini Tanzania kama wimbo bora wa mwaka wa Afro pop mwaka 2010, tuzo ya Chaguo la Teneez Music nchini Kenya kama wimbo ulioongoza kwa kuchukuliwa kwa njia ya mtandao Afrika Mashariki “The most downloaded East African song” mwaka 2010, pamoja na tuzo ya Nigeria Sound City Video Music kama wimbo bora wa Afrika Mashariki mwaka 2010.
Aliendelea kutayarisha nyimbo ambazo zilipata umaarufu mkubwa na kuingia kwenye vipengele mbalimbali vya tuzo za muziki za Kilimanjaro. Mwaka 2012, nyimbo tatu zilizotokana na mikono yake zilipata nafasi ya kushiriki tuzo hizo. Nyimbo hizo ni Liz One wa Izzo Business ambao uliingia kwenye vipengele viwili ambavyo ni wimbo bora wa mwaka na wimbo bora wa Hip hop na pia kusababisha msanii huyo aingie kwenye kipengele cha msanii bora wa Hip hop. Milele daima wa Barnaba na Kizunguzungu wa Rachel, ambapo zote ziliingia kipengele cha wimbo bora wa Zouk/Rhumba pia ni nyimbo alizotengeneza mtayarishaji huyo.
Nyimbo zingine alizotayarisha ambazo zilifanya vizuri kwenye vituo mbalimbali vya redio na TV ni Kisa pombe na Soldier za Mwasiti, Sorry sana, Mbayuwayu na Mtoto wa Afrika za Marlaw pamoja na Natumaini ya Becka aliyowashirikisha Barnaba na Amin. Pia zipo nyingine kama Unikimbie ya Amin, Tushukuru kwa yote ya Ditto, Lonely ya Linah na Magubegube ya Barnaba.
Mtayarishaji huyo ambaye hajawai kuingia kwenye tuzo za Kilimanjaro za muziki wa hapa nchini Tanzania ambazo mwaka huu zimeongezewa kipengele cha Mtayarishaji bora chipukizi ndiye aliyetayarisha wimbo wa Leka dutigite wa Kigoma All Stars kupitia Studio yake ya Ngoma Records. Wimbo huu umeingia kwenye kipengele cha wimbo bora wa mwaka 2013. Pia alishirikiana na mtayarishaji Imma the boy kutengeneza wimbo wa Me ‘n’ U wa Ommy Dimpoz ambao umeingia kwenye kipengele hicho na vipengele vingine ambavyo ni wimbo bora wa Bongo Pop na wimbo bora wa kushirikiana.
Alipoulizwa alisema hapendi kuzungumzia juu ya kutotajwa kama miongoni mwa wanaowania tuzo. Aliendelea kusema kwamba, hata kama baadae ikitokea, kwake ni motisha tu, lakini kikubwa zaidi ni kwamba anahisi analo deni kubwa la kutumia uwezo wake ipasavyo kufanya kazi nzuri zaidi ya hapo ili kuutangaza muziki wa Tanzania kimataifa. Pia alisema ana malengo makubwa aliyojiwekea na ndiyo maana kila kukicha anawaza kutayarisha nyimbo zenye tofauti na zenye radha ya kipekee.
Tudd Thomas anaendelea kukitumia kipaji chake na ujuzi wake ipasavyo na siku chache zilizopita kuna nyimbo zisizopungua tatu zilizoingia sokoni na zinafanya vizuri, ambazo ni kazi za mikono yake. Nyimbo hizo ni Uswazi take away ya Chegge, Nyumbani ya Kigoma All Stars na pia ameshirikiana kwa kiasi kikubwa na mtayarishaji Fundi Samwel kutengeneza wimbo wa Mahakama ya mapenzi wa Linex.

Comments