HARUNA MOSHI 'BOBAN' KUTIMKIA QATAR

ALIYEKUWA kiungo wa Simba, Haruna Moshi  ‘Boban’ anatarajiwa kutimkia Doha, Qatar kwa ajili ya kwenda kucheza soka la kulipwa katika klabu moja inayoshiriki ligi daraja la pili nchini humo. 
Akizungumza jijini Dar es Salaam juzi, mdau anayeshughulikia safari hiyo ambaye hakupenda kutajwa jina lake alisema kwamba tayari wameshatuma hati ya kusafiria ya mchezaji huyo nchini Qatar kwa ajili ya kupatiwa kibali cha kuingia nchini humo (viza). 
Alisema kwa asilimia kubwa safari ya mchezaji huyo imeiva na anatarajiwa kuondoka wakati wowote kuanzia sasa pindi viza hiyo itakaporejeshwa nchini. 
Aliongeza kuwa, kabla ya kusajiliwa mchezaji huyo kwanza atafanya majaribio kwa wiki kadhaa ili uongozi uweze kujiridhisha zaidi na kiwango chake. 
Iwapo nyota huyo atafanikiwa kusajiliwa na klabu hiyo itakuwa ni mara yake ya pili kwenda kucheza soka la kulipwa ambapo miaka ya nyuma alipata kusajiliwa na klabu ya Gefle IF ya nchini Sweeden kabla ya kuvunja nayo mkataba. 
Aidha, Boban ambaye amekuwa akitumika ndani ya klabu ya Simba kwa miaka kadhaa, kabla ua kumalizika kwa msimu uliopita wa ligi kuu bara alisimamishwa kwa muda usiojulikana kuitumikia klabu hiyo kutokana na utovu wa nidhamu yeye pamoja na beki, Juma Nyoso. 
Tayari uongozi wa Simba umetangaza kutomsajili tena Boban aliyemaliza mkataba wake. 
Katika hatua nyingine, kikosi cha Simba kilianza rasmi mazoezi jana chini ya kocha wake mpya Abdallah ‘King’ Kibadeni, amzoezi yaliyofanyika kwenye uwanja wa Kinesi jijini Dar es Salaam. 

Simba inatarajiwa kushiriki michuano ya klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati maarufu kama Kombe la Kagame inayotarajiwa kuanza kutimua vumbi Juni 18 hadi Julai 2 nchini Sudan ambapo leo kitaendelea na mazoezi yake asubuhi na jioni.

Comments