YANGA YAIVUA UBINGWA WA VPL SIMBA SC


Wachezaji wa Yanga wakishangilia moja ya bao jioni ya leo

VINARA wa ligi kuu ya Vodacom , Yanga Sc leo wameendelea kujiwekea mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa wa ligi hiyo baada ya kuwachapa mabao 3-0 maafande wa JKT Oljoro katika mchezo wa ligi hiyo uliopigwa kwenye uwanja wa Taifa.
Ushindi huo umeivua rasmi ubingwa Simba kwani Yanga imefikisha pointi 52 huku ikisaliwa na mechi tatu  ambapo kama itashinda itafikisha pointi  61  huku Simba inayoshika nafasi ya nne ikiwa na pointi 35 hata kama ikishinda mechi zake tatu zilizosalia itafikisha pointi 44 tu.
Kwa mantiki hiyo sasa mbio za ubingwa wa Ligi hiyo utawaniwa na Yanga pamoja na Azam Fc ambayo inashika nafasi ya pili ikiwa na pointi 46 na kusaliwa na mechi nne  ambapo ikishinda zote itafikisha pointi 52,lakini ubingwa wa Azam utategemea kama Yanga itapoteza mechi zake zilizosalia.
Katika mchezo wa leo, iliwachukua dakika ya tano Yanga kupata bao lao la kwanza  kupitia kwa Nadir Haroub ‘Canavaro’  aliyefunga kwa kichwa akiunganisha  kona ya Athuman Idd ‘Chuji’.Kona hiyo ilikuja baada ya kipa wa Oljoro kufanya kazi ya ziada kupangua shuti kali la Simon Msuva.
Dakika mbili baadaye, Hamis Kiiza alishindwa kuifungia Yanga bao akiwa na kipa baada ya kupokea pasi ya Simon Msuva aliyekuwa mwiba kwa walinzi wa Oljoro.
Dakika ya 19, Msuva aliipatia Yanga bao la pili kwa shuti la nje ya boksi baada ya kumlamba chenga beki wa Oljoro na jitihada za kipa wa Oljoro  Lucheke Musa kuokoa shuti hilo hazikuzaa matunda.
Didier Kavumbagu aliikosesha Yanga bao jingine katika dakika ya 24 baada ya kushindwa  kuitendea hali krosi ya Msuva, kabla ya dakika ya 32, beki wa Yanga Juma Abdul kuumia baada ya kugongana na winga wa Oljoro.
Dakika ya 36, Msuva alikosa bao baada ya shuti lake kutoka sentimiuta chache kwa juu, huku Yanga ikiutawala zaidi mchezo huo.
Hamis Kiiza aliipatia Yanga bao la tatu katika dakika ya 43 akitumia mpira mrefu kumzidi ujanja kipa wa Oljoro aliyetokea bila mafanikio.Hadi timu hizo zinakwenda mapumziko Yanga ilikuwa mbele kwa mabao 3-0.
Kipindi cha pili kilianza kwa timu kucheza mpira wa kutegeana kabla ya Oljoro kuanza kucheza rafu zisizo za msingi ambapo dakika ya 56, Emmanuel Memba alipewa kadi ya jnjano baada ya kumchezea rafu Kiungo wa Yanga, Haruna Niyonzima
Dakika ya 60 nyota wa kimataifa wa Yanga, Didier Kavumbagu aliumia na kushindwa kuendelea ambapo nafasi yake ilichulkuliwa na Said Bahanuzi
Katika mchezo huo pia, mchezaji wa Oljoro Majaliwa Sadik alizawadiwa kadi ya njano kwa kumchezea rafu Msuva
Dakika ya 87 kipa wa Oljoro alifanya kazi ya ziada kupoangua shuti la mbali la Nizar Khalfanm na kuwa kona tasa, kabla ya dakika tatu baadaye Bahanuzi kukosa bao la wazi baada ya kipa wa Oljoro kutokea na kupaisha juu.
Katika mchezo wa jana, Yanga iliwatoa Juma Abdul, Kavumbagu na Msuva  na kuwaingiza Shadrack Nsajigwa, Bahanuzi na Nizar Khalfan huku Oljoro ikiwatoa Kipa LKucheke, Karage Mgunda na kuwaingiza Shaibu Issa na Sixbert Mohammed.
Yanga: Ali Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul, David Luhende, Nadir Haroub ‘Canavaro’,Kelvi Yondan, Athuman Iddi ‘Chuji’,Simon Msuva, Frank Domayo,  Didier Kavumbagu na Haruna Niyonzima.
Oljoro:Lucheke Musa, Yusuph Machogoti, Majaliwa Sadiki, Nurdin Mohamed, Shaibu Nayopa, Salim Mbonde, Karage Mgunda, Emmanuel Memba, Paul Nonga, Idd Swaleh na Hamis Saleh. 

Comments