BOSI YANGA SC APEWA ONYO KALI


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), linatarajiwa kumlima barua ya onyo Makamu Mwenyekiti wa klabu ya Yanga, Clement Sanga(pichani), imefahamika.
Hatua hiyo inatokana na Sanga kudai kwamba TFF inataka kuihujumu klabu hiyo, baada ya kusogeza mbele mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya JKT Oljoro uliokuwa ufanyike juzi hadi kesho.
Shirikisho hilo lilifanya mabadiliko ya mchezo huo na ule wa Simba na Azam FC uliokuwa upigwe kesho kwenye Uwanja wa Taifa, ambao sasa utapigwa kesho kutwa, ili kutoa nafasi kwa mechi hizo kuoneshwa ‘live’ na kituo cha televisheni cha Super Sport.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah, alisema kwamba kauli ya Sanga ni upotoshaji mkubwa, kwani shirikisho hilo halipo katika kuhujumu timu yoyote, bali kuzisaidia klabu.
Alisema mechi kuoneshwa ‘live’ na kituo kikubwa kama Super Sport, inasaidia mambo mengi, ikiwamo kuzipa uzoefu wa kimataifa timu husika, pia kutoa fursa kwa wachezaji kuonekana katika nchi tofauti.
Yanga ambayo inaongoza ligi hiyo kwa pointi 49, ilitishia kutopeleka timu uwanjani baada ya mabadiliko hayo ya ratiba, kabla ya juzi kusalimu amri na kukubali kuingiza timu uwanjani.

Comments