Na Daudi Julian, Morogoro
Mafunzo elekezi ya siku mbili ya sheria 17 za soka
yanatarajia kufanyika machi 23 na 24, mwaka huu, mjini Morogoro.
Akizungumza na
mtandao huu, mratibu msaidizi wa mafunzo hayo, Fredrick Luunga alisema mafunzo
hayo yatashirikisha wadau mbalimbali wa mchezo wa soka katika Manispaa ya
Morogoro na kwamba yatafanyika katika ukumbi wa Mango.
Luunga aliwataja baadhi
ya wadau hao kuwa ni waamuzi wa mchezo huo, makocha, viongozi wa klabu,
wachezaji, waandishi wa habari za michezo pamoja na mashabiki wa kawaida.
Alisema
lengo la mafunzo hayo ni kuwawezesha wadau hao kuzijua ipasavyo na kuzitafsiri
vema sheria hizo.Mratibu huyo alisema mafunzo hayo yanafuatia utafiti wa muda
mrefu ambao amedai umebaini kuwa wadau wengi wa soka nchini hawazijui ipasavyo
sheria za mchezo huo na hivyo kuwa chachu ya vurugu katika mechi mbalimbali za
soka.
“Maandalizi kwa ajili ya mafunzo haya yanakwenda vizuri na tayari
tumeshaanza kutoa fomu kwa washiriki”, alisema.
Luunga alisema wakufunzi katika
mafunzo hayo ni wanaotambuliwa na chama cha waamuzi wa mpira wa miguu nchini
(FRAT) ambao amedai wana uwezo mkubwa wa kutafsiri sheria hizo.
Mratibu huyo
ametoa wito kwa wadau wa soka katika manispaa ya Morogoro kujitokeza kwa wingi
kwa lengo la kuchukua mafunzo hayo.
Alisema hiyo itawasaidia wadau hao kuzijua
sheria hizo na hivyo kuwa katika mazingira mazuri zaidi ya kuufurahia mchezo
huo.
Comments
Post a Comment