KOCHA Msaidizi wa timu ya Simba,
Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ amedai kuondolewa kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika
kulitokana na maandalizi hafifu na wachezaji hawapaswi kutupiwa lawama.
Mabingwa hao wa Tanzania, walijikuta
wakitolewa kwenye michuano hiyo na Recreativo do Libolo ya Angola kwa jumla ya
mabao 5-0. Awali ilifungwa bao 1-0 nyumbani kabla ya kutandikwa 4-0 ugenini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana,
Julio alisema timu yake haikupata maandalizi ya kutosha kwa ajili ya kushiriki
michuano ya kimataifa, tofauti na wenzao ambao waliipa umuhimu mkubwa michuano
hiyo.
Alisema, hali hiyo ndiyo ilisababisha kikosi
chake kuondolewa katika raundi ya kwanza tu, kitu ambacho ni cha kusikitisha na
kutia uchungu kwa timu kubwa kama Simba.
Julio aliongeza kuwa kutokana na
matokeo hayo, hakuna haja ya kuwatupia lawama wachezaji, kwani walijitahidi
kutimiza majukumu yao kwa kucheza kwa kiwango kinachostahili, lakini walizidiwa
na wapinzani wao.
Alisema matokeo yameshakuwa hayo, hivyo
kwa sasa hawana budi kuachana nayo na kuelekeza nguvu zao Ligi Kuu Bara ili
kuweza kujiweka katika mazingira mazuri zaidi.
“Tutahakikisha tunafanya maandalizi ya
hali ya juu ili tuweze kushinda michezo yetu iliyobaki na hivyo kupata nafasi
nzuri itakayotuwezesha kushiriki michuano ya kimataifa mwakani,” alisema.
Simba kwa sasa inashika nafasi ya tatu
ya ligi hiyo ikiwa na pointi 31 huku Azam
FC ikiwa ya pili na pointi 36 na Yanga inayoshikilia usukani ina pointi 42.
Katika hatua nyingine, uongozi wa Simba
jana ulikuwa na kikao na wachezaji kwa ajili ya kujadili mustakabali wa timu
yao, ambayo imekuwa na mwenendo mbaya katika mechi zake za hivi karibuni, zikiwemo
za mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara.
Habari zilizopatikana jana jioni
zinaeleza kwamba, Kamati ya Utendaji ya Simba, pamoja na viongozi wa Kamati ya Ufundi,
walikutana na wachezaji baada ya mazoezi ya jioni na kujadili kiini cha kufanya
kwao vibaya.
Kiongozi mmoja wa Simba, aliliambia Tanzania
Daima kwamba, lengo la kikao hicho ni kubaini tatizo ili kulitatua na
hatimaye kuondokana na mwenendo mbaya.
Hivi karibuni, kumekuwepo na ‘sintofahamu’
ndani ya klabu hiyo, ambapo kuna taarifa za mgomo wa chini chini unaofanywa na
wachezaji kwa madai ya kubaguliwa na baadhi ya viongozi, huku pia wakilalamikia
benchi la ufundi.
Comments
Post a Comment