WACHEZAJI SIMBA SC WAFICHUA SIRI YA KUFUNGWA KWAO


CHANZO cha kufanya vibaya kwa klabu ya Simba kwenye  michezo yake na hasa Ligi Kuu ya Vodacom inayoendelea hivi sasa nchini ni mgomo baridi unaondelea ndani ya kikosi cha timu hiyo, imefahamika. 
Mabingwa hao watetezi wa ligi hiyo wamejikuta wakipoteza ndoto zao za kutetea ubingwa wao baada ya kufanya vibaya kwenye michezo yake ya ligi hiyo ambapo kwa sasa wanashika nafasi ya tatu wakiwa na pointi 33 nyuma ya Azam Fc iliyo ya pili ikiwa na pointi 36 na vinara Yanga wenye pointi 39. 
Hali hiyo ilipelekea uongozi wa Simba chini ya Mwenyekiti wake Alhaj Ismail Aden Rage kuitisha kikao chja dharura mapema wiki hii ambapo moja ya maazimio yake ni kuitisha mkutano mkuu wa dharura wa wanachama ili kujadili suala hilo. 
Habari za kuaminika toka ndani ya klabu hiyo zinaeleza kwamba mgomo huo baridi unatokana zaidi na maslahi huku wakiwanyooshea vidole baadhi ya viongozi ambao wamekuwa chachu ya mgawanyiko huo. 
Immelezwa kuwa kuna baadhi ya viongozi wamekuwa wakionesha upendeleo kwa baadhi ya wachezaji wa timu hiyo hali ambayo si nzuri na hasa ikizingatiwa kuwa timu inaundwa na wachezaji wengi na si baadhi. 
“Unajua nini kwenye timu kuna wachezaji zaidi ya 25 sasa iweje kiongozi au viongozi waoneshe kuwajali wachezaji watano tu wakati kama shida na wengine pia wanashida, hii kitu haileti picha nzuri ndiyo maana hata morali imeshuka,”kilieleza chanzo hicho. 
Chanzo hicho kimeongeza kuwa ubaguzi huo wa kimaslahi unaofanywa na baadhi ya viongozi umekuwa ukiwaumiza sana wachezaji hao na kujiona hawana faida ndani ya klabu hiyo na matokeo yake kuamua kucheza bora liende tu. 
Mbali na hilo, inadaiwa kuwa maslahi  na hasa mishahara ya wachezaji  haijaongezwa kwa muda mrefu licha ya gharama za maisha kupanda kwa kasi sana kila kukicha. 
“Kuna wachezaji wanafamilia zinazowategemea, unampa mshahara huohuo kwa zaidi ya miaka mitatu unategemea nini wakati yeye maisha yake yanategemea kucheza mpira tu,”kilidai chanzo hicho.

Kwa upande mwingine inadaiwa kuwa wachezaji hao wanachanganywa na uwepo wa makocha wengi ndani ya timu kitu ambacho kinawafanya washindwe kufuata mafundisho ya nani.Simba ina makocha wanne, kocha mkuu Patrick Liewig, ambaye anasaidiwa na Jamhuri Kihwelo, Moses Basena na James Kisaka.

Akijibu shutuma hizo, ofisa habari wa Simba Ezekiel Kamwaga pamoja na alisema hizo ni sababu za kitoto sana kinachotakiwa ni kila mtu kutimiza jukumu lake lililompeleka kwenye klabu ya Simba. “suala la mshahara kila mtu lipo ndani ya mkataba aliousaini, pia kuna posho za kila siku kwenye mazoezi na mgawo wa mechi,”alisema

Kwa upande wa suala kuchanganywa kutokana na uwepo wa makocha wanne,  Kamwaga alisema halina mashiko kwani kila mtu ana kazi yake ambapo kuna kocha mkuu (Liewig), msaidizi (Kihwelo), Meneja (Basena) na Kocha wa makipa (Kisaka) na kudai kuwa wanaopaswa kuulizwa ni viongozi wa kamati ya ufundi ambao wana jukumu la kuushauri uongozi kuhusiana na masuala ya kiufundi.

“Vitu vingine vinashangaza sana hebu ona klabu kama Manchester United ina makocha karibu 20 na mambo yako vizuri, pia kila kocha yupo kwa kazi yake hivyo sidhani kama hili ni tatizo,”aliongeza

Comments