RAGE:SIJAJIUZULU, TUTATOA MAAMUZI MAZITO



KAMATI ya utendaji ya klabu ya Simba inatarajiwa kutoa uamuzi mgumu kuhusiana na mwenendo mbaya ulionayo timu hiyo katika ligi kuu ya Vodacom. 
Aidha, Mwenyekiti wa Simba, Alhaj Ismail Aden Rage amekanusha taarifa za kujiuzulu kwake kufuatia mwenendo mbaya wa timu hiyo kwenye ligi hiyo. 
Rage ameiambia Sports Lady leo kwamba kamati ya utendaji ya Simba itakutana leo hii kwa ajili ya kujadili mustakabali wa timu yao
Amesema  kikao hicho kitajadili kwa kina hali iliyopo sasa ambayo imesabababisha timu yao kupoteza hata matumaini ya kutetea ubingwa wao. 
“Tutakuna baadaye leo na kujadili hali hii maana tukiiacha hivi hivi inaweza kutuletea madhara makubwa sana…pia tutatoa maamuzi mazito baada ya kikao chetu,”alisema.
 Kuhusiana na taarifa za kujiuzulu kwake, Rage alisema anashangazwa na taarifa hizo zinapotoka kwani kama atafikia uamuzi huo ataitisha mkutano na waandishi wa habari na kuzungumzia hatua hiyo. 
“Mimi sijasema nitajiuzulu jamani hata hiyo taarifa yenyewe ukiisoma haileweki, hivyo nawaomba wanasimba kutulia kuona kipi kitakachofuata,”aliongeza Rage 
Simba imeonekana kusuasua sua katika ligi hiyo baada ya kutokuwa na matokeo ya kuridhisha sambamba na kuamulia vipigo katika mechi zake. 
Hali hiyo ilianza kujitokeza tangu mwishoni mwa mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo ambao ulipelekea kutoka kileleni hadi kushika nafasi ya tatu. 
Aidha, tangu kuanza kwa mzunguko wa pili wa ligi hiyo, Simba imeshinda mechi mbili dhidi ya African Lyon 3-1 na Tanzania Prisons 1-0, huku ikitoka sare mbili dhidi ya JKT Ruvu na JKT Oljoro kwa bao 1-1 kabla ya kufungwa bao 1-0 na Mtibwa Sugar jana.

Comments