MTIGINJOLA AZIDI KUMPOTEZEA MALINZI NA WENZAKE



KAMATI ya Rufani ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) chini
ya Mwenyekiti wake Idd Mtiginjola, leo  
ilitupa maombi ya kufanyia marejeo (review) uamuzi wake kwa waombaji watano waliokuwa wamechujwa.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mtiginjola alisema wamepitia Katiba ya TFF pia Kanuni za Uchaguzi za TFF na kubaini hakuna Ibara inayotoa fursa ya review kwa uamuzi uliofanyika.
Alisema kwa mujibu wa Kanuni za Mwenendo wa Madai (CPC) katika mahakama za kawaida, zinaruhusu Hakimu aliyefanya uamuzi katika kesi kufanya marejeo, lakini katika masuala ya soka hakuna fursa hiyo.
Kwa mazingira hayo, Mtiginjola amesema kamati yake haiwezi kujitungia kitu kipya kwani kazi yao ni kufanya uamuzi kwa kutafsiri Katiba na kanuni walizopewa
na mamlaka ya uteuzi, yaani TFF.
Waombaji watano waliokuwa wakitaka Kamati hiyo ifanyie marejeo uamuzi wake kutupa rufani zao ni Jamal Emil Malinzi aliyeenguliwa kugombea urais wa shirikisho hilo na wengine wanne.
Hao ni Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye kinyang’anyiro cha kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).
Wengine ambao waliomba kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF na Kanda zao kwenye mabano ni Eliud Peter Mvella (Iringa na Mbeya), Farid Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu).
Baada ya kuchujwa, Malinzi alimsihi Rais wa Shirikisho hilo, Leodegar Chilla Tenga kuingilia kati kutengua uamuzi huo.
Hata hivyo, mwishoni mwa wiki Tenga alisema hana uwezo huo, isipokuwa ni Kamati hiyo ya Rufaa kupitia upya jambo hilo.
Alisema kama mgombea atakuwa hajaridhika, bado anaweza kupeleka malalamiko yake Shirikisho la soka la Kimataifa (Fifa) na wao TFF watampa ushirikiano wa kutosha.
Zaidi ya hapo, Tenga alisema bado mgombea ana nafasi nyingine ya mwisho ya kuwasilisha malalamiko yake Mahakama ya Usuluhishi wa Masuala ya Michezo (Cas).
Tenga alisema hivyo ndivyo vyombo halali vinavyoweza kutoa haki na Shirikisho hilo likatoa ushirikiano kwa mhusika katika kupigania haki anayodhani amepokwa.
Aidha, kutokana na kuwepo kwa shinikizo la wagombea hao kutaka Kamati ya Mtiginjola kupitia upya uamuzi wake, Kamati ya Uchaguzi chini ya Deogratius Lyatto ametangaza kusitisha mchakato wa uchaguzi huo ambao ungefanyika Februari 24.
Kufanyika kwa uchaguzi huo ni baada ya uongozi wa Tenga aliyekalia kwa mara
ya kwanza kiti hicho Desemba 27, 2004 kumaliza muda wake na hatakitetea tena.   

Comments