LIUNDA, RWIZA KUSIMAMIA MECHI ZA LIGI YA MABINGWA




Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limewateua Watanzania Leslie Liunda na Alfred Rwiza kuwa makamishna wa mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika zinazoanza mwezi ujao. 
Rwiza ameteuliwa kuwa kamishna wa mechi kati ya APR ya Rwanda na Vital’O ya Burundi itakayochezwa nchini Rwanda kati ya Februari 15 na 17 mwaka huu. 
Naye Liunda atakuwa kamishna wa mechi ya marudiano kati ya Tusker ya Kenya na St. Michel United ya Seychelles itakayochezwa Kenya kati ya Machi 1 na 3 mwaka huu. Mechi zote ni za raundi ya awali.

WATANZANIA KUZICHEZESHA URA, COTTON SPORT
Waamuzi wanne wa Tanzania wameteuliwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kuchezesha mechi ya marudiano ya Ligi ya Mabingwa kati ya URA ya Uganda na Cotton Sport ya Cameroon itakayochezwa jijini Kampala kati ya Machi 1 na 3 mwaka huu. 
Orden Mbaga ndiye atakayekuwa mwamuzi wa kati na atasaidiwa na mwamuzi msaidizi namba moja Jesse Erasmo wakati mwamuzi msaidizi namba mbili ni Hamis Chang’walu. Mwamuzi wa mezani ni Israel Mujuni na Kamishna wa mechi hiyo atakuwa Souleiman Waberi wa Djibouti. 
Wakati huo huo, waamuzi kutoka Afrika Kusini ndiyo watakaochezesha mechi ya kwanza ya raundi ya awali ya Ligi ya Mabingwa kati ya Simba ya Tanzania na Clube Recreation Libolo ya Angola itakayofanyika Februari 17 mwaka huu jijini Dar es Salaam. 
Waamuzi hao ni Daniel Volgraaff atakayepuliza filimbi wakati wasaidizi wake ni Enock Molefe, Lindikhaya Bolo na Lwandile Mfiki. Kamishna wa mechi hiyo atakuwa Emmanuel Lesita kutoka Lesotho.

Comments