RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein,akisalimiana na Bi Fatma Baraka Khamis,(Kidude) baada ya kutunukiwa nishani ya Sanaa na Michezo na Rais wa Tanzania Dk.Jakaya Mrisho Kikwete,(kulia) katika sherehe za kutunuku Nishani katika Viwanja vya Ikulu Dar es Salaam,(katikati)Rais Mstaafu wa Tanzania Mzee Mwinyi.[Picha na Ramadhan Othman,Ikulu.]
Na Abdallah Khamis
MSANII mkongwe wa nyimbo za
taarab nchini, Fatma Baraka Khamis ‘Bi Kidude’, jana aliwaacha watu hoi katika
viwanja vya Ikulu jijini Dar es Salaam, aliposhindwa kwenda kupokea nishani ya
sanaa na michezo hadi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete,
alipoacha kiti chake na kumfuata na kumvisha.
Tukio hilo lilitokea jana wakati Rais Kikwete
alipokuwa akiwatunukia nishani watu mbalimbali kutokana na mchango walioutoa
kwa ajili ya maendeleo ya taifa kitaifa na kimataifa, ambapo jumla ya
wanamichezo watano walitunukiwa nishani hizo.
Wanamichezo wengine
waliotunukiwa nishani hizo mbali na Bi Kidude ni pamoja na Muhidini Gurumo,
mwanariadha mkongwe aliyejizolea sifa kitaifa na kimataifa, John Stephen
Akhwari, pamoja na Marijani Rajab na Fundi Said ‘Mzee Kipara’ ambao wote ni
marehemu.
Hali ya Bi Kidude kutaka
afuatwe alipokaa ilianza kuonekana mapema wakati watu waliokuwa wakitarajia
kutunukiwa nishani hiyo walipotajwa majina na kutakiwa kuinuka ambapo Bi Kidude
hakuinuka wala kupunga mkono hatua iliyozua minong’ono kuwa huenda bado
anaumwa.
Ilipofika wakati wa kwenda
mbele kupokea nishani, Bi Kidude aliendelea kuonesha usanii wake kwa kuamua
kuendelea kukaa kwenye kiti hadi alipofuatwa na kuvishwa nishani hiyo.
Wakati wa kwenda kupiga picha
ya pamoja kwa watu waliotunukiwa, Bi. Kidude aliinuka huku akiongozana na
Maalim Gurumo kwenda katika eneo lililopangwa kwa ajili ya picha hali
ilyowaacha watu hoi kwa kicheko.
Katika hatua ya kushangaza,
Bi. Kidude wakati akipongezwa na waandishi wa habari, badala ya kuwajibu
aliinua mkuno hewani na kutanua vidole viwili kisha akapeleka mdomoni kama ishara ya mtu anayevuta sigara kisha akaondoka
kwenda kukaa katika sehemu yake.
Comments
Post a Comment