KILI STARS KUCHEZA MECHI YAKE YA NUSU FAINALI ALHAMIS


Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars) itacheza nusu fainali ya michuano ya Kombe la Chalenji 2012 Alhamisi (Desemba 6 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Mandela ulioko Namboole jijini Kampala, Uganda. 
Kilimanjaro Stars ambayo itacheza mechi hiyo na mshindi wa robo fainali ya leo  kati ya wenyeji Uganda na Ethiopia imeingia hatua hiyo baada ya kuitoa Rwanda. Mechi imechezwa jana Uwanja wa KCC ulioko Lugogo, Kampala. 
Mabao ya Amri Kiemba dakika ya 33 na John Bocco dakika ya 53 ndiyo yaliyoifanya Kilimanjaro Stars itinge nusu fainali na kuifungisha virago Rwanda (Amavubi) inayofundishwa na Milutin ‘Micho’ Sredojovic kutoka Serbia. 
Vijana wa Kilimanjaro Stars wanaonolewa na Kim Poulsen walitawala pambano hilo, hasa kipindi cha kwanza kwa pasi fupi fupi. Kilimanjaro Stars imefungwa bao moja katika mechi nne ilizocheza tangu michuano hiyo ilipoanza Novemba 24 mwaka huu jijini Kampala. 
Kilimanjaro Stars ambayo katika michuano hiyo iliyofanyika Dar es Salaam mwaka jana iliishia hatua ya nusu fainali iliwakilishwa na; Juma Kaseja, Erasto Nyoni, Amir Maftah, Shomari Kapombe, Kelvin Yondani, Amri Kiemba, Salum Abubakar/Athuman Idd, Frank Domayo, Mwinyi Kazimoto, John Bocco na Mrisho Ngasa.

Comments