FM ACADEMIA YAWAITA KESHO KUKATA KEKI YA MIAKA 15

 mratibu wa onyesho la miaka 15 ya fm academia Nassib Mahinya na Nyoshi El Saadat


MASHABIKI wa muziki wa dansi nchini ,wameombwa kujitokeza kwa wingi kwenye onyesho maalum la maadhimisho ya miaka 15 ya bendi ya muziki wa dansi nchini Fm Academia ‘Wazee wa Ngwasuma’ litakalofanyika kesho kwenye ukumbi Msasani Club. 
Akizungumnza na waandishi wa habari jana kwenye hoteli ya Southernsun jijini Dar es Salaam, Rais wa bendi hiyo, Nyoshi El Sadat alisema wamejipanga vema kuhakikisha wanatoa burudani ya uhakika. 
Alisema kuwa kupitia onyesho hilo, wanataka kuonyesha thamani waliytonayo mashabiki wa bendi hiyo na muziki wa dansi kwa ujumla kupitia burudani ya nguvu. 
“Litakuwa ni zaidi ya onyesho kwani miaka 15 kwa bendi kuwa imesimama si kitu kidogo, lakini kikubwa ni kuwashukuru mashabiki wetu kwa kutufanya tuwe juu tangu mwaka 1997 mpaka sasa,”alisema. 
Nyoshi aliongeza kuwa, pamoja na burudani ya aina yake ambayo itahusisha nyimbo zao kuanzia za albamu ya kwanza, Hadija mpaka zile zilizopo kwenye albamu yao ya saba, pia wasanii waliowahi kupitia bendi hiyo watapata kupanda jukwaani. 
Naye mratibu wa onyesho hilo, Nassib Mahinya kupoitia kampuni ya Sinai Entertainment alisema maandalizi yamekamilika ambapo kiingilio kitakuwa sh 10, 000 kwa kila mmoja ambacho kitamuwezesha kupata chupa moja ya bia ya Windhoek Lager. 
Alisema mbali na FM Academia pia kutakuwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali wakiwemo Dogo Janja, PNC na kundi la Mapacha Watatu. 
Onyesho hilo limedhaminiwa na Mabibo Beer Wine & Spirit, Mama Mbaga Catering, Africa Media Group, Chonapi General Supplier, Benny Mlokozi Company , Big Solution, Mtanashati Entertainment, Eliado Point View, Arafa Salon, Friendship Restaurant, Saluti5.com, Tigo na  Masters Club.

Comments