NSAJIGWA ATEMWA KIKOSI CHA YANGA KAGAME


Kocha mkuu wa Yanga Tom Saintfiet akizungumza na waandishi wa habari leo wakati akitaja kikosi cha wachezaji wa timu hiyo watakaoshiriki michuano ya Kagame, kushoto ni kaimu meneja wa bia ya Kilimanjaro Oscar Shelukindo na kulia ni Katibu Mkuu wa Yanga, Mwesiga Selestine.

WAKATI michuano ya kombe la Kagame ikitarajiwa kuanza kutimua vumbi kesho, kocha mkuu wa mabingwa watetezi wa michuano hiyo, Mbelgiji Tom Saintfiet ametangaza silaha atakazotumia katika michuano hiyo huku akimuengua nahodha wa timu hiyo, Shadrack Nsajigwa ‘Fuso’ . 
Saintfiet pia amewaacha kwenye kikosi hicho wachezaji nyota chipukizi watatu wakiwemo Simon Msuva, Omega Seme na Frank Damayo. 
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Saintfiet pamoja na kumsifu  Nsajigwa kuwa ni mchezaji mzuri na muhimu, alisema ameamua tu kutomjumuisha katika michuano hiyo badala yake  atamtumia katika Ligi Kuu soka Tanzania Bara. 
Kuhusiana na wachezaji chipukizi, kocha huyo alisema  watakuwa na majukumu ya kitaifa na timu ya Taifa ya Vijana wenye umri chini ya miaka 20 inayojiandaa na mchezo wake wa kufuzu fainali za mataifa ya Afrika dhidi ya Nigeria, itakayopigwa Julai 29. 
“Kanuni zinanitaka kuachia wachezaji siku tano kabla ya mechi na hawa vijana watarudiana na Rwanda Jumatatu kabla ya kuanza kujiandaa na mechi yao na Nigeria…nasikitika kutokuwa nao lakini sina jinsi,”alisema. 
Kocha huyo ambaye ameteua wachezaji kwa kushirikiana na wasaidizi wake Fred Felix Minziro na Mfaume Athuman, pia amewaacha katika kikosi xchake wachezaji nyota kama Nurdin Bakari na Salum Telela kutokana na kukabiliwa na majeruhi. 
Akizungumzia michuano hiyo, Sainfiet alisema ni migumu kwani timu nyingi zinazoshiriki zimetoka katika Ligi tofati na Yanga ambayo ilikuwa mapumziko kwa muda mrefu na kuanza mazoezi hivi karibuni lakini anaimani na kikosi chake. 
“Kwa siku chache nilichokuwa nancho nimebainia vipaji na hata mchezo wetu wa kirafiki na JKT Ruvu Jumanne wachezaji walitimiza wajibu wao ipasavyo hivyo nataraji mambo mazuri zaidi katika Kagame,”alisema. 
Kocha huyo aliongeza kuwa ana imani kubwa na wachezaji wake kwani pia wana nindhamu ya ndani na nje ya uwanja, hivyo ana uhakika wataweza kushinda mataji muhimu ambayo waliyakosa mwaka jana. 
Aliongeza kuwa, Yanga inahitajki kushinda mchezo wake wa kwanza dhidi ya Atletico na hivyo kujiweka katika nafasi nzuri ya kutinga hatua ya robo fainali ya michuano hiyo. 
Aliwataja wachezaji hao ni pamoja na makipa Yaw Berko na Ally Mustafa ‘Barthez’, mabeki Juma Abdul, David Luhende, Kelvin Yondan, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Godfrey Taita, Ladislaus Mbogo, Oscar Joshua na  Stefano Mwasyika.

Kwa upande wa viungo ni pamoja na Athumani Iddi ‘Chuji’, Rashid Gumbo, Juma Seif ‘Kijiko’, Haruna Niyonzima, Shamte Ally, Nizar Khalfan, Idrisa Assenga, Hamisi Kiiza na washambuliaji Said Bahanuzi na Jerry Tegete. 
Naye kaimu meneja wa bia ya Kilimanjaro inayozidhamini timu za Simba na Yanga,  Oscar Shelukindo alisema kampuni ya bia Tanzania (TBL) itaendelea kuwa bega kwa bega na timu hizo Simba katika kuhakikisha inashiriki kikamilifu mashindano hayo. 
Shelukindo amezitaka timu hizo kujibidiisha ili kuhakikisha zinalibakisha kombe hilo hapa nchini ambapo Yanga itaanza kampeni hiyo kesho kwa kukwaanza na Atletico ya Burundi, huku Simba itaianza Jumapili kwa kukwaana na URA ya Uganda. 
Mbali na Simba na Yanga, michuano hiyo pia itashirikisha timu za Azam Fc, Mafunzo ya Zanzibar  APR ya Rwanda, El Salam Wau ya Sudan Kusini,  Vita Club ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na Ports ya Djibouti 

Comments