DAMU YA SIMBA YAMKOSESHA NYOSO MAMILIONI YA YANGA


RASMI, dili la Juma Said Nyosso kutua Yanga limekufa, baada ya kujiridhisha beki huyo ni ‘Simba damu’, ila sasa mazungumzo na mshambuliaji wa Daring Motema Pembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Mussa Hassan Mgosi yameanza rasmi.
Kutoka ndani ya Yanga,zinaeleza kwamba  klabu hiyo haina mpango kabisa wa kumsajili Nyosso na wamemtaka Mwenyekiti wa Simba, Alhaj Ismail Aden Rage awe na amani.
Hivi sasa Yanga inaumiza kichwa kupata beki wa kati kutoka nje ya Tanzania atakayekuwa akisaidiana kazi na Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Yondan. Aidha, Yanga inafuatilia kama kweli kiungo mkabaji, Shaaban Mussa Nditi amesaini Coastal Union ya Tanga au la ili ijaribu kumsajili.
Wachezaji wengine ambao Yanga inawatolea macho ni nyota wa Mtibwa Sugar Said Bahanuzi ‘Ortega’ na Hussein Javu- ambao wote wana mikataba na timu hiyo ya Manungu.
Tayari kutoka kikosi cha msimu uliopita wachezaji wazawa Nsajigwa Shadrack, Kiggi Makassy, Bakari Mbega, Abuu Ubwa na Zuberi Ubwa wamekwishatemwa.

Comments