WANACHAMA YANGA SASA WATAKA MKUTANO MKUU

HALI ndani ya klabu ya Yanga imeendelea kuwa tete baada ya jana wanachama kuutaka uongozi wa klabu hiyo chini ya Mwenyekiti wake Lloyd Nchunga kuitisha mkutano mkuu wa wanachama kwa mujibu wa katiba.
Hatua hiyo inafuatia kesi iliyofunguliwa Septemba 4,2011 katika mahakama ya hakimu Mkazi Kisutu  na wanachama Kingwaba Kingwaba, Juma Matimbwa na Siwema Chiokota kufutwa.
Akizungumza na mamapipiro blog leo, mmoja ya wanachama wa klabu hiyo akiwakilisha kundi la vijana Bakili Mohammed Makele alisema kwamba wamefikia hatua hiyo baada ya kuona mambo ndani ya klabu hiyo yanaharibika hivyo mahala pa kupatikana jibu ni katika mkutano mkuu.
Alisema uongozi wa Nchunga umeshindwa kuitisha mkutano huo kwa kivuli cha kusingizia uwepo wa amri hiyo ya mahakama kitu huku akiambatana na baadhi ya wanachama mahakamani kushinikiza mkutano huo kuendelea kusimamishwa, lakini ukweli ni kwamba  amri hiyo ililenga mkutano wa Septemba 4 tu.
Aliongeza pamoja na kutafuta mahala pa kuongelea matatizo yao wanataka taarifa za mapato na matumizi ya klabu, masuala ya mikataba na mambo mengineyo ambayo ni muhimu na wanachama wana haki ya kuyafahamu.
“Tunachohitaji ni mkutano mkuu wa wanachama ili tupate pa kusemea yanayotusibu, klabu yetu inaenda mrama, tunahitaji mapato na matumizi na hata kujua mikataba waliyoingia viongozi,”alisema.
Makele aliongeza kuwa wanachama hawana mpango wa kumuondoa madarakani Nchunga kama anavyohofia kwa sasa, kikubwa ni kufuata  katiba ya Yanga na soka kwa ujumla na hasa ikizingatiwa uongozi haujawahi kufanya mkutano tangu uingie madarakani mwaka juzi.

Naye mwanachama Said Bakari alisema kuwa Nchunga anadhalilisha taaluma ya Wanasheria kutokana na kutofuata katiba ya Yanga na soka kwa ujumla katika kuongozi hivyo hana budi kushitakiwa hata kwa Shirikisho la soka Tanzania (TFF) .

“Yanga imepoteza mwelekeo kutokana na viongozi wachache kufanya mambo kinyume na katiba, hali hii mbaya sana na inazidi kuipeleka pabaya klabu, tunaomba sana tena sana mwenyekiti wetu Nchunga aitishe mkutano,”alisema Bakari.

Comments