WAJUMBE YANGA WAMSHINIKIZA NCHUNGA KUJIUNZULU


WAKATI wajumbe wa kamati ya utendaji ya klabu ya Yanga wakizuia kujiuzulu kwa mwenzao Mohammed Bhinda (pichan), badala yake wajumbe hao walimtaka mwenyekiti wa klabu hiyo Lloyd Nchunga kujiuzulu.
 Maamuzi hayo yalifikiwa juzi katika kikao cha kamati ya utendaji ya Yanga kilichoketi kwa ajili ya kujadili mustakabali mzima wa hali tete inayoendelea ndani ya klabu hiyo, pamoja na barua ya masharti waliyopewa na aliyekuwa mfadhili wa klabu hiyo Yusuf Manji.
 Habari zilizopatikana toka ndani ya kikao hicho zinaeleza kwamba, baada ya Bhinda kuwasilisha barua yake ya kujiuzulu, wajumbe hao wakiongozwa na Salum Rupia walizuia zoezi hilo kwa madai ya kwamba kiongozi huyo ni muhimili mkubwa ndani ya uongozi huo.
 Imeelezwa kuwa, pamoja na kugoma huko, wajumbe hao walidai kuwa ni heri Nchunga ajiuzulu kwani ndiye anayelalamikiwa zaidi na wanachama wa klabu hiyo lakini si Nchunga hivyo kumshauri aachie ngazi.
 Mmoja ya wajumbe hao alieleza kwamba baada ya kumsauri Nchunga kuachia ngazi aliwaomba  wampe siku mbili au tatu afikirie zaidi ushauri huo kabla ya kutolea uamuzi.
 “NI kweli tulizuia barua ya kujiuzulu kwa Bhinda kwani bila yeye hakuna lolote katika uongozi wa Yanga na tulimshauri Nchunga ajiuzulu kwani matatizo yote hayo na kelele kutoka kwa wanachama vinamlenga yeye,”alisema mjumbe mmoja.
 “Kama tusipomshauri afanye hivyo itakuwa ngumu kufanuikisha mambo mengi ambayo yanaikabili timu yetu yanayohitajika kufanyika haraka iwezekanavyo na kwa hali yake ya kuendelea kuwepo ndani ya Yanga kutafanya mambo yaendee kuwa magumu zaidi,”aliongeza .
 Kikao hicho kilihudhuriwa na wajumbe wachache baada ya wengi wao kutangaza kubwaga manyanga kutokana na kuchoshwa na hali ya sintofahamu inayoendelea ndani ya klabu hiyo, ambapo tayari  Makamu Mwenyekiti Davis Mosha, pamoja na wajumbe Seif Ahmed, Ali Mayay, Bhinda na  Mzee Yusuf  walitangaza kung’atuka
 Kwa sasa Yanga imebaki na wajumbe wanne, wakimo  Sarah Ramadhani,Tito Osoro, Charles Mgondo, na Salum Rupia.
 Hata hivyo, Nchunga ambaye jumapili iliyopita alivuliwa madaraka hayo na wanachama zaidi ya 700 waliokutana makao makuu ya klabu hiyo iliyopo mitaa ya Jangwani na Twiga, hakupatikana kuzungumzia suala hilo baada ya simu yake kuita bila kupokelewa.
 Hivi karibuni, uongozi wa Yanga ulijikuta katika msigano na wanachama wa Yanga wakiongozwa na baraza la wazeee na baadhi ya vijana wakitaka ujitoea madarakani kutokana na kushindwa kuiletea mafanikio timu hiyo ambayo ilijikuta ikiutema ubingwa wake wa ligi kuu bara ulionyakuliwa na mahasimu wao Simba na yenyewe kuishia nafasi ya tatu. 
Aidha, uongozi huo unadaiwa kushindwa kuwalipa wachezaji pamoja na viongozi wa benchi la ufundi hatua ambayo imepelekea benchi la ufundi kuachia ngazi, huku klabu hiyo ikiwa mbioni kutaifishwa na mahakama kuu baadhi ya mali zake kutokana na deni la milioni 106. 
Tayari Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) lilikemea mapinduzi yaliyofanywa na wanachama wa Yanga kwa madai ya kukiuka kanuni, huku wakidai kutotambua mapinduzi hayo na kuwataka wanachama hao kutumia busaya katika kutatua suala hilo. 
Hata hivyo, wazee hao wametishia kuifuta Yanga TFF na kuihamishia Visiwania Zanzibar, pia kuwasilisha ombi maalum kwa taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) ili imchunguze Nchunga kwa madai kuwa huenda kuna ubadhirifu anaoufanya ndiyo maana hataki kung’oka Yanga.


Comments

  1. Mpendwa tupo pamoja, ni hapa na pale twashukuru kwa taarifa hii

    ReplyDelete

Post a Comment