NMB, SBL WAIPIGA JEKI TWIGA STARS


WAKATI timu ya Taifa ya soka ya Wanawake ‘Twiga Stars’ inaondoka kesho  kwenda Ethiopia Kampuni ya Bia Serengeti (SBL)  kwa kushirikiana na Benki ya NBM, wameichangia timu hiyo kiasi cha sh.Twiga Stars’ Sh. Milioni 30 ili kuiwezesha timu hiyo. 
Twiga Stars itaondoka  kwa ndege ya Ethiopian Airlines kwenda Addis Ababa kwa ajili ya  mechi ya mchujo ya Fainali za Afrika kwa Wanawake (AWC) dhidi ya Ethiopia, itakayopigwa Mei 27 mwaka huu.
 Akizungumza leo katika makabidhiano hayo, yaliyofanyika kwenye hosteli za  Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),  Mkurugenzi wa Masoko wa SBL, Ephraim Mafuru alisema kwamba wameamua kutoa mchango huo baada ya kuombwa na serikali kuisaidia kutokana na kutokuwa na mdhamini.
 Alisema wao wametoa Sh. Milioni 15 na NMB nayo imetoa kiwango kama hicho, sambamba na vifaa vya michezo vikiwemo jezi, viatu, soksi, suti na vinginezo vyote vikiwa na thamani ya shilingi mil.5.5.
 “Kwa kuzingatia umuhimu wa kuisaidia timu hiyo, tulikutana na NMB, ambao walikuwa wadhamini wenzetu katika timu ya soka ya wanaume, Taifa Stars kabla ya kujitoa mwaka jana na tukakubaliana kuisaidia Twiga kwa kiwango hicho”, alisema.
 Naye Meneja Masoko wa NMB, Imani Kajula alisema kwamba kama wadau wakubwa wa michezo wameona umuhimu wa kuisaidia timu hiyo na pia kuanzisha kampeni ya kuitafutia misaada zaidi.
 Alisema wamefungua akaunti inayoitwa; Changia Twiga Stars na amewataka wadau na makampuni mengine kuichangia timu hiyo kupitia akaunti hiyo ambapo anaamini kutokana na benki yao  kuwa na matawi mengi nchini, itakuwa rahisi kwa wadau mbalimbali kuisaidia timu hiyo.
 Kwa upande wake, Kocha Msaidizi wa timu hiyo, Nasra Juma Mohamed pamoja na kuwashukuru SBL na NMB kwa msaada huo, aliahidi matokeo mazuri katika mechi yao hiyo.
 HAta hivyo,Nasra alisema Watanzania wasikatishwe tamaa na matokeo mabaya ya mechi zao mbili za majaribio kwani zimewapa ari kubwa na kuwasaidia kwa kiasi kikubwa kuona ni sehemu gani wanahitaji kuifanyia marekebisho kabla ya kuivaa Ethiopia.
 Nasra pia aliwashukuru Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Dioniz Malinzi walioitembelea timu hiyo kambini juzi  na kutoa posho ya siku 16 kwa wachezaji na makocha wa timu hiyo.

Awali, Mkurugenzi wa Ufundi wa TFF, Sunday  Kayuni alisema timu hiyo inakabiliwa na hali mbaya kifedha hivyo  TFF ikaamua kusaka wafadhili kwa kushirikiana na serikali na akawashukuru SBL na NMB kwa kujitokeza, huku akiyaomba makampuni mengine kujitokeza kuisaidia timu hiyo ili iweze kufuzu kwa mara ya pili mfulululizo kucheza fainali hizo.
 Msafara wa Twiga Stars utakaokuwa na watu 25 wakiwemo wachezaji, benchi la ufundi na viongozi utaagwa kesho saa saa tano asubuhi kabla ya kuondoka saa 11 jioni chini ya Mwenyekiti wa Chama cha soka cha  Wanawake Tanzania (TWFA) ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF, Lina Kessy.
 Twiga Stars itarejea nyumbani Mei 28 mwaka huu kusubiri mechi ya marudiano itakayochezwa Juni 16 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Mshindi ndiye atakayepata tiketi ya kucheza Fainali za Nane za AWC zitakazochezwa Novemba mwaka huu nchini Equatorial Guinea.

Comments