NCHUNGA:SIJIUZULU NG'O

LICHA ya baraza la wazee wa klabu ya Yanga kumtaka mwenyekiti wao Lloyd Nchunga ajiuzulu, mwenyekiti huyo amesema ataendelea na majukumu yake kama mwenyekiti halali wa Yanga. Jana, baraza la wazee wa Yanga kupitia kwa katibu wake Ibrahim Akilimali lilitoa siku sita kwa Nchunga na wajumbe wa kamati ya Utendaji Yanga kuachia ngazi kinyume na hapo watashusha mvua ya masika. Wazee hao pia walidai kuwa wamefikia uamuzi huo kutokana na uongozi wa Nchunga kushindwa kuongoza na hivyo kuisababishia klabu matatizo mbalimbali, hivyo hata kikao cha wazee alichokiitisha Mei 20 kinashangaza kwa kuwa aliwakana na kusema katiba ya Yanga haina wazee, hivyo wao wameona siku hiyo iwe ni kwa ajili ya mkutano mkuu wa wanachama wote, huku akiwaomba wanachama kujitokeza kwa wingi ili kushuhudia Nchunga akijiuzulu. Nchunga ameiambia mamapipiro blog kwamba anashangazwa na shinikizo hilo la kumtaka kujiuzulu wakati anaongoza klabu hiyo kwa mujibu wa katiba ambayo ndiyo ilimuweka madarakani. Alisema yeye kama mwenyekiti alikutana na wajumbe wa kamati yake ya utendaji na kujadili matatizo yote wanayodai wanachama hao na ndiyo maana alitoa majibu kupitia kwenye vyombo mbalkimbali vya habari. Baadhi ya masuala aliyoeleza Nchunga ni pamoja tarehe ya kikao baina yake na wazee wa klabu hiyo, mkutano mkuu wea wanachama, mchakato wa usajili pamoja na kutafuta kocha mpya kutoka nchi mbalimbali duniani. “mimi sifanyi mambo kwa shinikizo, nafuata katiba ya Yanga inasema nini, hivyo tarehe 20 Mei nimepanga kukutana na wazee, na mkutano mkuu wa wanachama ni Julai 15, kama kuna mengine nje na niliyoamua na viongozi wa kamati ya utendaji sina mamlaka nayo,”alisema.

Comments