NCHUNGA KUFIKISHWA TAKUKURU, YANGA KUHAMISHIWA ZANZIBAR


SIKU moja baada ya Shirikisho la soka Tanzania (TFF) kukemea msigano uliopo baina ya baadhi ya wanachama wa klabu ya Yanga na uongozi wa klabu hiyo, wazee wa klabu hiyo wameibuka na kuitaka taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) kumchunguza mwenyekiti wake, Lloyd Nchunga.
Aidha, wanachama hao wametishia kujifuta uanachama klabu hiyo TFF na kwenda kuisajili kwa chama cha soka Visiwani Zanzibar (ZFA). 
Hatua hiyo inafuatia wanachama wa klabu hiyo zaidi ya 700 kumng’oa madarakani Nchunga jumapili iliyopita kutokana na kutoridhishwa na utendaji wake. 
Katibu wa baraza la wazee la Yanga Ibrahim Akilimali, ameiambia mamapipiro blog  kwamba wanaandaa maelezo maalum ili kuweza kuyawasilisha TAKUKURU ili waweze kumchunguza Nchunga kwani kuendelea kwake kung’ang’ania madaraka kunaonyesha kuwa si muadilifu. 
“Tunajipanga kuwasilisha maelezo TAKUKURU ili wamchunguze Nchunga kwani inaonekana mwenzetu huyu anafanya hujuma kubwa ambazo zinamfanya ang’ang’anie kuwepo Yanga,”alisema. 
Alisema wamekerwa na TFF kuendelea kumkumbatia Nchunga kwani pamoja na kuanza kumlalamikia muda mrefu kiongozi huyo amekuwa akikwepa matakwa ya wanachama wa klabu hiyo ambayo kwa sasa imeathirika kutokana na utendaji wake mbovu. 
Aliongeza iwapo TFF itaendele kumkumbatia Nchunga watachukua jukumu la kuifuta uanachama wake na kwenda kujisajili Zanzibar kwani ni bora kwenda kucheza ligi visiwani Zanzibar kuliko Tanzania bara. 
Jana, TFF  kupitia kwa katibu wake mkuu Angetile Osiah ilieleza kutotambua mapinduzi yaliyofanywa na wanachama wa Yanga kwani lipo katika kusimamia katiba kwa wanachama wake wote, huku akiwataka wanachama wa Yanga kutumia busara zaidi katika kudai haki zao za kikatiba. 
Alisema kuwa wanachama wa Yanga walipaswa kusubiri Mkutano Mkuu uliopangwa na Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo Julai 15, mwaka huu na kufanya maamuzi wanayoyataka lakini si kuitisha mikutano bila kufuata katiba.

Comments

  1. Dina Ismail
    Jana katika pitia pitia blogs tofauti nilibahatika kusoma kitu flani kuhusiana mgogoro wa wanayanga na ningependa wajue kitu hichi kabla ya mahamuzi makubwa wanayotaka kuyafanya....


    NAWAKUMBUSHA TU AL SHABAAB 700, NCHUNGA ALISHINDA KWA KURA 1,437


    ETI wanachama 700 wa Yanga walikutana Jumapili makao makuu ya klabu, makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam na kufikia uamuzi wa kumng’oa madarakani Mwenyekiti, Wakili Lloyd Bahargu Nchunga.
    Mapinduzi haya yaliongozwa na Mzee Ibrahim Akilimali, ambaye kihistoria nilishasema siku nyingi ni mzee kinara wa migogoro na mvuruga amani klabuni.
    Kweli, Nchunga ameshindwa kuongoza Yanga na sababu kubwa ni uelewa wake mdogo katika masuala ya michezo na kukosa ushirikiano kutoka kwa Wajumbe wenzake wa Kamati ya Utendaji na wadau wengine wa klabu, wakiwemo hao wanaojiita wazee.
    Lakini ukirejea uchaguzi uliomuweka madarakani Nchunga Jumapili ya Mei 18, mwaka 2010, alishinda Uenyekiti baada ya kupata kura 1,437, akiwaangusha wapinzani wake wanne, Francis Kifukwe aliyepata kura 370, Mbaraka Igangula aliyepata kura 305, Abeid Falcon aliyepata kura 301 na Edgar Chibura aliyeambulia kura 65 katika kura 2,220 zilizopigwa, wakati kura 23 kati ya hizo ziliharibika.
    Kura 370 za Kifukwe na 305 za Igangula kwa pamoja wakichanganya, bado hawawezi kufikia kura za Nchunga- ina maana alishinda kwa kishindo. Inakuwa rahisi kuhisi watu hawa 700 waliokutana Jumapili ni wale wale 700 waliomnyima kura Nchunga PTA Mei 18, 2010.
    Sitaki kuzama ndani sana- kwa sababu nimeshapitisha sera ya kutoandika habari za migogoro- lakini kwa pamoja na wasomaji wangu napenda tujadili, kiongozi aliyeshinda kwa kura 1,437 anaweza kung’olewa madarakani na watu 700?
    Tena watu ambao hakuna aliyewahakiki kama kweli ni 700 na hakuna aliyehakikisha kama kweli ni wanachama wa Yanga? Tujadili.

    NAOMBA UIWEKE WAZI ILI KILA ANAYEJIITA MWANA YANGA ATAMBUE HILI........

    festchrist

    ReplyDelete

Post a Comment