MISS DAR INTERCOLLEGE KUANZA KUJINOA LAMADA KESHO


WAREMBO watakaoshiriki shindano la Miss Dar Intercollege 2012  kesho wanatarajiwa kuanza mazoezi ya kujiandaa na shindano hilo kwenye hoteli ya Lamada, jijini Dar es Salaam. 
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, mratibu wa shindano hilo Dina Ismail alisema jana kwamba warembo hao watatoka vyuo vya  Biashara (CBE), Uandishi wa Habari (DSJ) na Time, pamoja na  Ustawi wa Jamii. 
“Kesho (leo) tutaanza mazoezi yetu pale Lamada ambapo warembo kutoka vyuo vinne wataanza kujinoa…wiki ijayo huenda tukaongeza washiriki wengine ambao watatoa chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) ambao wanafanya shindano lao mwishoni mwa wiki hii,”alisema. 
Alisema kuwa warembo hao watakuwa chini ya ukufunzi wa  mrembo aliyepata kushiriki shindano hilo, Rose John, huku kwa upande wa shoo watanolewa na Bob Rich. 
Dina aliwataja wadhamini waliojitokeza mpaka sasa ni pamoja na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia bia ya Redd’s, Lamada Hotel, Ndege Insurance, na  Dodoma Wine, huku akiomba makampuni mengine kujitokeza kudhamini shindano hilo litakalofanyika mwezi ujao.

Comments