TFF YAIPONGEZA SIMBA KWA KUSONGA MBELE

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa uongozi, benchi la ufundi na wachezaji wa Simba kwa kufanikiwa kuingia raundi ya pili (hatua ya 16 bora) ya michuano ya Kombe la Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).
Bila shaka juhudi, ushirikiano kutoka kwa wadau mbalimbali, wachezaji kujituma na kuzingatia maelekezo kutoka kwenye benchi la ufundi la timu hiyo linaloongozwa na Milovan Cirkovic ndiyo msingi wa mafanikio ya Simba.
Tunaamini ushindi huo wa Simba ni changamoto kubwa kwa wachezaji na viongozi kuhakikisha timu hiyo inafanya vizuri zaidi katika michuano ya kimataifa kwa vile ina uwezo huo.
Licha ya Simba kufungwa 3-1 na ES Setif jana (Aprili 6 mwaka huu) mjini Setif imefanikiwa kusonga mbele katika michuano hiyo kwa faida ya bao la ugenini. Simba ilishinda mechi ya kwanza nyumbani mabao 2-0.
Katika hatua ya 16 bora, Simba itacheza na mshindi wa mechi kati ya El Ahly Shandy ya Sudan na Ferroviario de Maputo ya Msumbiji. Timu hizo zilitarajia kurudiana kesho (Aprili 8 mwaka huu) nchini Sudan.
Simba itacheza mechi ya kwanza Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, Aprili 29 mwaka huu wakati ya marudiano itakuwa ugenini kati ya Mei 11, 12 na 13 mwaka huu.
Powered by Sorecson : Creation de site internet
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Comments