TENGA ADAIWA KUITENGA ZANZIBAR


WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Dk Mwinyihajji Makame amesema kwamba rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Chillah Tenga anavuruga Muungano katika michezo kwa kuitenga Zanzibar.
Katika mahojiano maalum na bongostaz.blogspot.com mchana huu katika hoteli ya Zanzibar Beach Resort visiwani hapa, Dk Makame amesema kwamba TFF ya Tenga imekuwa ikichukua maamuzi mengi mazito kuhusu masuala ya soka yenye kugusa maslahi ya pande zote mbili, bila kuwashirikisha ZFA (Chama cha Soka Zanzibar).
Dk Makame ametolea mfano muundo wa timu ya taifa, Taifa Stars kuanzia uteuzi wa kocha na hata suala la udhamini wa timu, Zanzibar huwa hawashirikishwi jambo ambalo amesema ni baya ni linahatrisha muungano katika michezo nchini.
Dk  Makame amesema kwa sasa anasikia timu ya taifa inataka kubadilishwa jina kutoka Taifa Stars na kuwa Kili Stars, jina ambalo linatokana bia ya wadhamini wapya Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) na anakitika maamuzi hayo yanachukuliwa bila Zanzibar kushirikishwa.
“Siungi mkono suala la Taifa Stars kubadilishwa jina, naomba Wizara husika zote mbili, zisimamie hilo lisijitokeze,”alisema.
Dk Makame, ambaye pia ni Mlenzi wa timu ya Ikulu SC amesitikishwa na kitendo cha TFF kutoikumbuka ZFA katika migawo wanayopata kutoka FIFA.
Aidha, Dk Makame alisema kwamba muundo wa TFF pia unapaswa kurekebishwa, ili uendane na muundo wa serikali mbili katika nchi hii.
“Kuna serikali ya Muungano na serikali ya mapinduzi, katika serikali ya mapinduzi tuko wenyewe kwa sababu tunasimamia mambo yetu tu huku, lakini serikali ya Muungano ipo kwa ajili ya taifa letu zima, inahusisha watu wa pande zote mbili. Utaona Rais anatoka Bara, lakini Makamu wake anatoka Zanzibar.
Vivyo hivyo, katika muundo wa Baraza la Mawaziri pia, unahusisha pande zote mbili, lakini ndani ya TFF, Zanzibar haihusishwi kabisa, hii si sawa na matokeo yake soka ya huku inazidi kudidimia kwa sababu hatunufaiki hata migawo ya FIFA,”alisema.
“Tunampenda sana Tenga, tangu akiwa mchezaji, Kocha na sasa kiongozi, rais wa TFF, CECAFA na anaiwakilisha vema nchi yetu kwa kweli, ila lazima ahakikishe anatenda haki,”alisema.
Aidha, kwa upande wake Naibu Waziri wa Habari Utamaduni Utalii na Michezo, Bi Hindi Hamad Khamis amelaani vikali pia desturi ya TFF kuitenga ZFA.
Bi Hindi, ameiambia bongostaz.blogspot.com mchana huu katika hoteli ya Zanzibar Beach Resort visiwani hapa kwamba anasikia hivi sasa timu ya taifa inataka kubadilishwa jina na kuwa Kili Stars wakati timu hiyo ni ya muungano na ZFA hawajashirikishwa.
“Si haki kutoishirikisha ZFA ndani ya TFF, lazima kuwe na ushirikiano kama tulionao kwenye serikali yetu ya Muungano.
Bi Hindi alipoulizwa kama amefanya jitihada zozote za kukutana na Wizara inayohusika na Michezo katika serikali ya Jamhuri ya Muungano, alisema; “Unajua hivi karibuni yamefanyika mabadiliko ya Baraza la Mawaziri huku kwetu, ila Waziri aliyepita hakika alifanya hivyo na mimi napenda niwaahidi wapenzi wa michezo Zanzibar na Wazanzibari kwa ujumla, kwamba tutafuatilia,”alisema Bi Hindi.
Naye Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi jimbo la Raha Leo (CCM), Nassor Salim Ali ‘Al Jazeera’ amelaani vikali pia kitendo cha TFF kutoishirikisha ZFA katika masuala ya soka yenye kugusa maslahi ya pande zote mbili.
Al Jazeera aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa ZFA Wilaya ya Mjini Magharibi, alisema kwamba naye amesikia juu ya mpango wa timu ya taifa kutaka kubadilishwa jina na kuwa Kili Stars, lakini anapinga.
“TFF hawawezi kubadilisha jina la timu ya taifa inayoihusisha na Zanzibar pia, bila kuishirikisha ZFA, hii si sawa na mbaya zaidi jina lenyewe ni la pombe kitu ambacho kipo tofauti na sisi kimaadili yetu,”alisema.
Al Jazeera alisema Zanzibar wamekuwa wakijitahidi kulinda Muungano katika michezo na ndiyo maana kila mwaka katika Kombe la Mapinduzi hualika timu za Bara.
Lakini amesema anasikitika TFF au Bara kwa ujumla wanaitenga Zanzibar. “Timu ya taifa ni yetu sote, lakini haiji kucheza huku hata mechi za kirafiki, wakati sisi tunakuwa wenyeji wa michano mikubwa tu ya CECAFA hapa. Tunakosaje sifa za kuandaa mechi ya timu ya taifa, japo ya kirafiki?”alihoji Al Jazeera.
Vigogo hawa wanatoa malalamiko hayo, katika wakati mwafaka kwani ni leo Mkutano Mkuu wa TFF umeanza katika ukumbi wa NSSF Water Front, Dar es Salaam na unatarajiwa kufungwa kesho.
CHANZO:BONGO STAZ BLOG

Comments