SIMBA, SHENDY WAKAMIANA KESHO


Kocha mkuu wa Simba Milovan Cirkovic kushoto akizungumza na waandishi wa habari leo kuhusaina na mechi yao na Al Ahli Shendi ya Sudan kesho, kulia ni mkuu wa msafara wa Shendi, Gamer Aldin Osman na kati ni ofisa habari wa TFF, Boniface Wambura.

WAWAKILISHI wa Tanzania katika kombe la Shirikisho barani Afrika (CAF) Simba kesho  wanashuka katika dimba la Taifa jijini Dar es Salaam kukipiga na Al Ahli Shendi ya Sudan katika mchezo wa kwanza wa 16 bora ya michuano hiyo. 
Kocha mkuu wa Simba Mserbia Milovan Cirkovic ameiambia mamapipiro blog kwamba kikosi chake kipo katika hali nzuri na amekiandaa vema ili kiweze kushinda mchezo wa huo ili kujiweka katika mazingira mazuri. 
Hata hivyo, Msebia huyo alishindwa kuahidi kama timu yake itaibuka na ushindi zaidi ya kusisitiza kuwa amekiandaa vizuri kikosi chake na hasa kupitia michezo ya ligi kuu soka Tanzania bara.
 “Siwezi kuahidi ushindi kesho lakini kikubwa ni kwamba nimekiandaa vema kikosi chake hivyo ni matarajio yangu tutafanya vizuri katika mchezo wetu huo,”alisema. 
Aidha, Milovan aliongeza kuwa mechi hiyo inatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa na hasa ikizingatiwa kuwa kila mmoja atahitaji kushinda ili kujiweka katika mazingira mazuri kwenye mechi ya marudiano. 
Naye mkuu wa msafara wa  Shendi, Gamer Aldin Osman Siza, pamoja na kukiri kutoifahamu Simba, alisema wamejipanga vema kuhakikisha wanashinda ugenini na hatimaye kwenda kumalizia kazi nyumbani watakaporudiana. 
Alisema mchezo huo unatarajiwa kuwa mgumu kutokana na wapiunzani wao nao kuhitaji ushindi wa nyumbani hivyo dakika 90 ndizo zitaamua nani zaidi ya mwenzake. 
Al Ahly wanakutana na Simba baada ya kuitoa Ferroviario ya Msumbiji kwa jumla ya mabao 3-0, huku Simba iliitoa Es Setif ya Algeria huku Simba ikibebwa na bao la ugenini baada ya nyumbani kushinda 2-0 kabla ya kwenda kufungwa 3-1. 
Mechi hiyo itachezeshwa na  waamuzi  kutoka nchini Swaziland Nhleko Simanga Pritchard, Mbingo Petros Mzikayifani,Sibandze Thulani,  Fakudze Mbongiseni Elliot na Kamishna wa Kayijuga Gaspard wa Rwanda. 
Mgeni rasmi katika mechi hiyo anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye ambaye ni mmoja ya wadau wakubwa wa klabu hiyo. 

Comments