NUSURA SEMTAWA ATAMBIA LIMBWATA

MUIGIZAJI wa filamu hapa nchini, Nusura Semtawa ‘Vick’, amejigamba kuwa, picha yake mpya inayokwenda kwa jina la ‘Limbwata’ itakuwa gumzo mitaani kutokana na nyota wake kufanya mambo makubwa.
Nusura ambaye kwa sasa anaishi nchini Uingereza, alitanabaisha kuwa filamu yake hiyo ni ya pili, huku akibainisha filamu yake ya kwanza, inayokwenda kwa jina la ‘Damu ya Mjomba’ hadi leo ikiwa ni zaidi ya miaka miwili, bado msambazaji hajaitoa.
Aliongeza kuwa ustadi katika kuandaa filamu hiyo ni moja ya msukumo mkubwa unaomfanya aamini kwamba ‘Limbwata’ itakuwa kivutio kwa mashabiki wa ndani na nje ya nchi.
“Filamu hii ni stori nzuri na inasisimua sana, kwani inazungumzia jinsi baadhi ya wanaume wanavyozitelekeza ndoa na familia zao, kwa kuhamia kwa hawara baada ya kulishwa dawa za kimapenzi ‘Limbwata’,” alijinasibu Nusura.
Aidha, alisema anaamini asilimia 100 ‘Limbwata’ italeta mapinduzi makubwa kwa waigizaji katika kuandaa filamu na kuzipa majina ya hapa nyumbani, ukilinganisha na hivi sasa ambako nyingi zimekuwa zikiitwa kwa majina ya kigeni.
Nusura, aliwataja nyota walioshiriki katika filamu hiyo kuwa ni pamoja na Nurudin Mohammed ‘Chekibudi’, Jerry Mshana ‘Jerry’, Snura, Salome na wengineo.

Comments