MWAKALEBELA AWANG'ATA SIKIO WAJUMBE WA MKUTANO MKUU WA TFF



Na Mwandishi wetu
WAKATI  mkutano mkuu wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF) unatarajiwa kufanyika kesho, Katibu Mkuu wa zamani wa shirikisho hilo, Fredrick Mwakalebela amewashauri wajumbe kujadili masuala ya kulipatia uwezo  shirikisho hilo na kuepuka kuwa tegemezi. 
Mwakalebela amesema kuwa  TFF inaweza kuepukana na hali ya kuomba fedha kwa wadau ili kusafirisha timu ya Taifa ya wanawake na baadala yake kutengeneza sera itakayowafanya wadhamini washindani kudhamini timu na shughuli mbali mbali bila kuingilia shughuli za mwengine. 
Alifafanua kuwa  udhamini wa kampuni ya simu ya Vodacom unawazuia kampuni nyingine za simu kama Tigo, Zantel na Airtel kudhamini timu shughuli nyingine za shirikisho hilo na kunyimwa fursa ya kuendeleza michezo nchini. 
Mwakalebela alisema kuwa TFF inatakiwa kuandaa sera ambazo zitawaruhusu wadhamini kama hao kudhamini hata timu za taifa za vijana na wanawake ili watanzania waweze kufaidi matunda ya uwekezaji wao. 
Katibu Mkuu huyo pia alitoa ushauri  kwa wajumbe hao kujadili suala la matumizi ya uwanja wa kumbukumbu ya Karume kutumika kibiashara zaidi kutokana na ukweli kuwa upo katika eneo zuri (Prime Area) kwa ajili ya shughuli hiyo na kuwaingizia kipato. 
Alisema kuwa eneo hilo linaweza kutumika kwa ujenzi wa maduka, hotel na vitega uchumi mbai mbali ambavyo vitaiondolea shirikisho hilo uhaba wa kupata fedha kwa ajili ya shughuli zake mbali mbali mbali. 
Kuhusiana na kushuka kwa soka la Tanzania, Mwakalebela aliwaomba wajumbe kujadili na kuweka mikakati mikubwa ya kuanzisha soka la vijana wadogo  kwa kushirikiana na Cecafa, CAF na Fifa ili kufikia lengo. Alisema kuwa kwa kuandaa vijana hao, wataweza kushindana katika mashindano ya vijana na baadaye kufanya vyema kwa upande wa soka la wakubwa. 
“Kwa sasa soka la vijana lipo jijini Dar es Salaam, Zanzibar  na pengine Arusha, mikoa mingine ni sawa na hakuna na hii inatokana na changamoto za maeneo ya kuchezea, hivyo mipango thabiti inatakiwa kuwekwa ili kufanikisha hilo,” alisema. 
Vile vile Mwakalebela aliwataka wajumbe hao kujadili maenedeleo ya soka la wanawake kwa kupanua wigo na kuiwezesha mikoa mengine nao kuwa na timu za wanawake na syo kutegemea Dar es Salaam tu na hasa Kinondoni. 
Alisema kuwa soka la wanawake limeonyesha kuwa ndilo linaweza kuitoa Tanzania kimasomaso kimataifa.

Comments