MBUNGE AIVUA NGUO'TFF



MBUNGE wa Ziwani, Ahmed Juma Ngwali (CUF), amelishukia Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kuwa limejikita kuendeleza migogoro, majungu, fitina na ubinafsi.
Ngwali, alieleza hayo bungeni mjini hapa jana, alipokuwa akiuliza swali la nyongeza na kuongeza kuwa, shirikisho hilo linasumbuliwa na ugonjwa wa woga, kukosa dira, muono na utamaduni wa kifikra, katika kuendeleza soko nchini.
Kutokana na hali hiyo, alihoji serikali ina mkakati gani wa kuendeleza soka nchini?.”
Aidha, alitaka jina la shirikisho hilo libadilishwe, kwa madai kuwa, linahusu Tanzania Bara pekee na liitwe Tanzania Mainland Football Federation (TMFF).
“Kwa mujibu wa Katiba, Ibara ya kwanza na ya pili, Zanzibar ni sehemu ya Muungano na kwa kuwa, Katiba ya TFF inatambua mikoa 21 ya Tanzania Bara na haitambui mitano ya Zanzibar. Je, serikali haioni haja kulibadilisha jina na kuliita TMFF?” alihoji mbunge huyo.
Naibu Spika, Job Ndugai, kabla ya kumruhusu Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, kujibu swali hilo, alihoji kama ni kweli mkakati wa chombo hicho ni kuendeleza migogoro na fitina.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri huyo alisema, hakuna haja ya kulitambulisha shirikisho kuwa ni la Bara pekee, kwa kuwa TFF inashirikiana na ZFA na kuwa hakuna mtafaruku.
“Dhana ya kutaka kuleta mgawanyiko si sahihi,” alisema.
Kuhusu madai dhidi ya TFF, Dk. Mukangara alisema, kazi yake kubwa ni kutatua migogoro na kuongeza kuwa kumekuwapo migogoro katika vyama vya mipira na jukumu la shirikisho hilo ni kuitatua.
Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Kapteni mstaafu, George Mkuchika, alisema kampuni nyingi zinatumia jina la Tanzania kwa sababu kuacha kutumia jina la Tanganyika.
“ Mtuelewe, kutumia jina hili ni kwa ridhaa kati ya ZFA na TFF na hakuna mgogoro wowote juu ya matumizi ya jina hili. Yako maelewano ya kutosha baina ya TFF na ZFA,” alisema.
Aliongeza kuwa, hitilafu ndogo ndogo zilizokuwepo, yalifanyika makubaliano na serikali ikafanya jitihada ya kuwakutanishwa na kuunda kamati ya pamoja ya kuzimaliza.
Akielezea ushirikiano uliopo, alisema, vyama hivyo viliwahi kupeleka ujumbe FIFA, kwenda kudai haki ya ZFA kuwa mwanachama wa shirikisho hilo.
Aidha alisema misaada inayotolewa kwa TFF kutoka FIFA, sehemu hugawiwa kwa ZFA, kama ambavyo ilifanyika kwa fedha za kukarabati uwanja wa michezo wa Gombani, Pemba.
 “Msimamo wa TFF ni kuendelea kuungana na wenzetu wa Zanzibar, kudai uanachama wa FIFA kwa Zanzibar, ili misaada iongezeke na nchi yetu inufaike,” alisema Mkuchika aliyewahi kuwa waziri mwenye dhamana na michezo.

Comments