KIPINDI CHA LUNINGA ‘MWANA DAR ES SALAAM’ KUZINDULIWA RASMI ‘DAR LIVE’ APRIL 28, 2012.


 Mkurugenzi wa Masoko na Ukuzaji wa Biashara wa Benki ya BPZ kutoka Zanzibar Bw. Juma Hafidhi (kushoto) akizungumza machache kwa niaba ya benki hiyo, ambapo amesema benki yao imeona umuhimu mkubwa wa kudhamini uzinduzi wa kipindi hicho kwani manufaa yake ni muhimu kwa jamii ambayo ndio wateja wao.  Katikati ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Palatte Media Co Ltd Bw. Redemptus Masanja na kulia ni Mmiliki wa Maduka ya Hussein Pamba Kali Bw. Hussein Maulid.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Palatte Media Co Ltd Bw. Redemptus Masanja akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na uzinduzi wa Dokumentari ya Kwanza ya kipindi cha luninga cha "MWANA DAR ES SALAAM itakayoitwa 'SAFARI YA NUNGWI'. Katikati ni Mkurugenzi wa Masoko na Ukuzaji wa Biashara wa Benki ya BPZ kutoka Zanzibar Bw. Juma Hafidhi.

Vyombo husika nchini vimetakiwa kutoa mafunzo kwa jamii kuhusu usalama wao wawapo safarini na jinsi ya kujiokoa pindi majanga yanapotokea iwe majini na hata barabarani.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa dokumentari ya kwanza ya kipindi kipya cha luninga kiitwacho ‘MWANA DAR ES SALAAM’ Mkurugenzi wa Kampuni ya Palatte Media Co Ltd Bw. Redemptus Masanja amesema kipindi hicho kitakuwa kikitangazwa na mtangazaji maarufu Mussa Hussein.
Amesema sehemu ya kwanza ya kipindi hicho imepewa jina la ‘SAFARI YA NUNGWI’ na kuwa imekusanya taarifa mbali mbali kuhusu tukio zima la kuzama kwa meli ya MV Spice Islander, iliyozama katika kina cha bahari cha mita 350 wakati ikitoka Unguja kuelekea kisiwani Pemba mnamo Septemba 10, 2011 na kuacha msiba kwa taifa.
Amefafanua kuwa kipindi cha ‘MWANA DAR ES SALAAM’ kitakuwa kimebeba masuala mbali mbali ya kijamii, kiuchumi na kisiasa na kitafanya uchambuzi wa kina katika matukio mbali mbali yaliyotokea au yanayoendelea kutokea nchini.
Kipindi hicho kinachoandaliwa na kampuni ya Palatte Media Co Ltd na kutangazwa na Mussa Hussein kitakuwa kikirushwa mara mbili kwa wiki katika luninga ya Clouds TV siku ya Jumapili Saa 1 jioni na kurudiwa siku ya Jumanne Saa 9 Alasiri na Ijumaa Saa 12 jioni.
Kipindi cha televisheni cha ‘MWANA DAR ES SALAAM’ kitazinduliwa rasmi tarehe 28 April 2012 katika hafla itakayofanyika katika ukumbi wa ‘Dar Live’ uliopo Mbagala jijini Dar es Salaam.
Bw. Hafidhi pia amesema PBZ katika kuonyesha inawajali wateja wake ambao pia ni wasafiri wa kati ya Zanzibar na Dar es Salaam kila siku, benki hiyo imefungua matawi mawili, moja likiwa katika Benki ya Kiislam ya PBZ ambalo linapatikana katika mtaa wa Lumumba na Mahiwa na tawi jingine ni la Conventional Bank ambalo linapatikana mtaa wa Swahili na Mkunguni. 
Katika kuhakikisha wananchi wanafurahia huduma zao, benki ya PBZ ni mwanachama katika Mtandao wa ATM ya Umoja Switch ambao utawasaidia wateja wake hasa wale wafanyabiashara kupata huduma ya kutoa fedha popote waendapo.
Aidha ametoa wito kwa wafanyabiashara haswa wanaosafiri kati ya Dar es Salaam na Zanzibar au Dar es Salaam kwenda mikoa mingine ya Tanzania kuweka fedha zao katika matawi yao yaliyopo Dar es Salaam na kuweza kuzitoa kwa kutumia mashine za ATM pindi wanapofika huko waendako, badala ya kusafiri na lundo la fedha.

Comments