KAMUA SIMBA KAMUA ITAMBAE


WAWAKILISHI wa Tanzania kwenye michuano ya Afrika, Simba SC ya Dar es Salaam leo wanashuka kwenye Uwanja wa Mei 8, mjini Setif kumenyana na wenyeji ES Setif katika mechi ya marudiano, Raundi ya Pili Kombe la Shirikisho Afrika.
Ikiwa na hazina ya ushindi wa mabao 2-0 katika mchezo wa kwanza, wiki iliyopita Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam- Simba inahitaji hata sare yoyote ili kusonga mbele na hata ikitokea bahati mbaya ya kufungwa, isiwe zaidi ya 1-0.
Ikitokea Simba ikafungwa 2-0, mchezo huo utahamia kwenye dakika 30 za nyongeza na kama matokeo yatabakia kuwa sare, basi mikwaju ya penalti itachagua timu ya kusonga mbele.
Tishio kubwa la Simba katika mchezo wa leo ni hali ya hewa ya baridi kali mjini Setif na Mwenyekiti wa Simba, Alhaj Ismail Aden Rage alisema jana kwamba wataandaa kahawa ili wachezaji wa timu hiyo wawe wanapewa wakati wanacheza uwanjani ili kupunguza baridi.
Rage pia alisema amenunua glavu na fulana za mikono mirefu wachezaji wavae ndani ya jezi katika mechi hiyo, ili kupambana na baridi kali la nchi hiyo ya Kaskazini mwa Afrika.
Mitaa ya jiji la Setif, Simba walikuwa wakionyeshewa alama ya vidole vitatu hadi vitano kila walipokatiza- ikiwa ni ishara kuelekea mechi ya leo.
Mapema jana, Kocha Mkuu wa Simba, Milovan Cirkovic, alisema hali ya hewa ya mji wa Setif ambayo ni baridi kali inaweza kuwa faida kwa timu yake na si hasara.
Milovan alisema hali ya hewa ya baridi huwafanya wachezaji wasichoke mapema tofauti na joto ambalo huchosha.
Kuna baridi za aina mbili. Kuna baridi inayotokana na hali ya hewa ya mahali na kuna baridi inayotokana na eneo kuwa kwenye miinuko (altitude). Zote ni baridi lakini zina tofauti.
“Ile ya miinuko huwafanya wachezaji washindwe kupumua vizuri na huwa na athari mbaya sana. Tuliliona hili kwenye mechi ya Kiyovu lakini hapa Setif hakuna miinuko sana kama Rwanda na hivyo watu wanaweza kucheza vizuri,”alisema.
Alisema jambo la muhimu kwa timu yake ni kutoathiriwa na sauti za washangiliaji wa Setif wala kughadhabika kirahisi wanapochokozwa na wapinzani wao.
“Mechi yetu na Setif ni ngumu sana. Kila timu ina nafasi ya kufanya vizuri ingawa sisi tuna faida kutokana na ushindi tulioupata nyumbani. Ni jukumu letu kuhakikisha tunaulinda ushindi wetu,” alisema.
Simba jana ilipewa fursa kwa mujibu wa kanuni za Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kufanya mazoezi kwenye Uwanja wa Mei 8 na walionekana kuufurahia Uwanja huo wenye nyasi bandia.
Mazoezi ya jana yalikuwa ya kwanza kufanywa na Simba katika mji huu wa milima milima na hali ya hewa ilikuwa ya baridi kali kwa kiwango cha nyuzijoto tisa.
Simba walianza mazoezi katika uwanja huo majira ya saa 12:30 kwa saa za hapa sawa na saa mbili na nusu usiku huko, na mazoezi hayo yalifanyika kwa muda wa masaa mawili na nusu.
Wachezaji wote wa Simba walihudhuria mazoezi hayo ambayo kama kawaida yalikuwa chini ya uangalizi wa benchi la ufundi na yalihudhuriwa na Watanzania waliokuja kuisapoti timu, wananchi wa Setif na askari waliokuwa wakiangalia mazoezi hayo na kulinda usalama.
Kabla ya Simba kufanya mazoezi, uwanja huo ulitumiwa na timu ya Setif kwa mazoezi pia na ilibidi wachezaji wa Simba wasubiri nje ya uwanja kwa takribani dakika 45, kabla ya kuruhusiwa kuingia.
Kwa upande wake, Nahodha wa Simba, Juma Kaseja, alisema vitimbi wanavyofanyiwa na wenyeji havitawafanya wapunguze ari ya kushinda pambano lao dhidi ya Setif kesho.
Kaseja alisema wametazama kwa makini matukio mbalimbali yanayofanywa na wenyeji wao na wamebaini yako mambo ambayo lengo lake ni kuwaondoa mchezoni.
“Hebu fikiria, watu wanataka kutusafisha kwa basi kwa masaa sita wakati wanajua kanuni ni masaa mawili tu. Halafu, badala ya kutusafirisha hadi mji wa Setif tulipocheza, wao wametupeleka kwanza mji mwingine na halafu wakatusafirisha kwa basi kuja Setif. Hizi ni mbinu zao lakini tunazijua,”alisema.
Kaseja alikuwa miongoni mwa wachezaji wa Simba walioitoa Zamalek ya Misri katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika miaka kumi iliyopita na anasema hakuna cha ajabu iwapo timu yake itaitoa Setif.
“Katika uzoefu wangu wa soka, timu pekee ya kiarabu ambayo ilitutendea vema ilikuwa ni Harass Al Hadoud ya Misri miaka miwili iliyopita. Lakini hawa walikuwa wema kwa sababu walikuwa wametufunga katika mechi ya kwanza na hivyo hawakuwa na wasiwasi.
“Ukiona Waarabu wanakufanyia vitimbi ujue wana wasiwasi na wewe. Kama hawana hofu, watakupa kila unachohitaji. Nashukuru kwamba tuna wachezaji wazoefu wa kutosha wanaoweza kupambana na lolote,” alisema.
Setif inakuwa timu ya tatu kihistoria kumenyana na Simba SC, baada ya awali Wekundu hao wa Msimbazi kutolewa na JET katika Klabu Bingwa Afrika, kabla na wao kuitoa Al Harrach katika Robo Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika.
Kwa ujumla Simba ni mabalozi wazuri wa Tanzania katika michuano ya Afrika na wamekuwa wakifanya vema kila wanapomenyana na timu kutoka Kaskazini mwa Afrika.
Kuelelea mchezo huo, bongostaz.blogspot.com inakuletea rekodi ya Simba na timu za Kaskazini mwa Afrika, zikiwemo za kutoka Algeria. Mungu ibariki Simba. Ibariki Tanzania.

REKODI YA SIMBA NA WAARABU:
LIGI YA MABINGWA AFRIKA:
MWAKA 1974:
NUSU FAINALI:
Simba Vs Mehallal 1-0: 0-1
(Mehalla ilishinda kwa penalti 3-0, ingawa kuna habari za kipa wa Simba, Athumani Mambosasa (sasa marehemu) kufanyiwa fujo, wakati wa upigwaji wa penalti.

MWAKA 1981:
RAUNDI YA PILI:
Simba ilitolewa na JET ya Algeria.

MWAKA 2003:
RAUNDI YA PILI:
Simba (Dsm) Vs Zamalek 1-0
Zamalek (Misri) Vs Simba 1-0
(Simba ilifuzu kwa penaliti 3-2)
MECHI ZA KUNDI A:
Sept. 7/2003: Simba Vs Ismaili 0-0
Sept. 19/2003: Ismaili (Msri) Vs Simba 2-1

KOMBE LA WASHINDI
MWAKA 1985
RAUNDI YA PILI
Simba SC Vs Al Ahly (Misri) 2-1 0-2

MWAKA 1996
RAUNDI YA PILI
Simba Vs Al Mokaoulun (Misri) 3-1 0-2 3-3 (Al Mokaoulun walifuzu kwa faida ya bao la ugenini)

MWAKA 2001
RAUNDI YA PILI
Ismailia (Misri) Vs Simba SC 2-0, 0-1, 2-1
(Mechi ya marudiano ilichezwa mara mbili, baada ya mechi ya kwanza kuvunjika dakika ya 46, SImba ikiwa inaongoza mabao 2-0, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam(sasa Uhuru). Ismailia walilalamikia hali ya Uwanja kujaa maji kwamba kutokana na mvua kubwa iliyonyesha siku hiyo, hivyo kugoma kucheza katika mazingira yale na mchezo ukasogezwa mbele kwa siku moja na ndipo wenyeji waliposhinda 1-0. Hivyo Simba kwa kufungwa 2-0 awali mjini Cairo, walijikuta wakitolewa kwa matokeo ya jumla ya kufungwa 2-1.
Mchezo wa kwanza ulitawaliwa na vurugu, Polisi walivamia uwanjani kuwatawanya wachezaji wa Ismailia kwa mabomu ya machozi, waliokuwa wakimzonga refa kwa madai mashabiki wa Simba walimpiga na chupa mchezaji mwenzao mmoja, Emad El-Nahhas.

KOMBE LA CAF/SHIRIKISHO:
MWAKA 1993
ROBO FAINALI:
Simba Vs USM El Harrach (Algeria) 3-0 0-2 3-2

MWAKA 2010:
RAUNDI YA PILI:
Aprili 25: Simba Vs Haras El Hodoud 2-1
Mei 8: Haras El Hodood Vs Simba SC 5 – 1

MWAKA 2012
Machi 25, 2012: Simba SC 2-0 ES Setif
Aprili 6, 2012; ES Setif Vs Simba SC .

Comments

  1. Mmeishapigwa tatu..kelele tu, historia wa waarabu nini...mmetoka sasa, sijui mtaongea nini...nyinyi kalieni soccer la bongo...sisi tuna enjoy mpira wenyewe hapa Uingereza....

    ReplyDelete

Post a Comment