WANACHAMA SHIWATA KUKUTANA KESHO


Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Habari Utamaduni na Michezo, Dkt. Emmanuel Nchimbi atakuwa mgeni rasmi katika mkutano mkuu wa Mtandao wa Wasanii Tanzania (SHIWATA) ambao utafanyika ukumbi wa StarLight, Dar es Salaam Jumamosi (kesho) Machi 31, 2012 kuanzia saa 4 asubuhi.
Katika  mkutano huo wanachama watapata taarifa kuhusu mikakati ya awamu wa pili ya ujenzi wa nyumba 178 kati ya 1,000 zinatarajiwa kujengwa katika kijiji cha Mwanzega, Mkuranga.
Mwenyekiti wa SHIWATA, Caasim Taalib alisema ,paka sasa imejenga nyumba tano(5)za awali kwa gharama ya sh. 33,789,097 ambapo mbili kati ya hizo tayari zimekabidhiwa kwa wanachama Josephine Moshi na Flora Kafwembe.
Alisema nyumba hizo ambazo zimejengwa kwa tofali za kupachika na nyingine kwa tofali za saruji zimeezekwa kwa vigae vya kisasa kutoka Wakala wa Taifa wa Utafiti na Ujenzi wa Nyumba za Gharama Nafuu (NHBRA) ambazo zimekuwa kivutio kikubwa katika kijiji cha Mwanzega, wilayani Mkuranga kiasi cha kufafanishwa na kijiji cha Hollywood ya Marekani na kukibatiza kijiji hicho kuwa cha Tanzawood.
Mwenyekiti Taalib alisema mpaka sasa makampuni mbalimbali za nchini pamoja na wafadhili kutoka Saudi Arabia ni baadhi ya wafadhili walionesha nia ya kuchangia ujenzi wa kijiji hicho.
Alisema mpaka sasa viongozi mbalimbali wamefika kuona ujenzi wa nyumba hizo ambazo zimepewa baraka na Wizara ya Habari Utamaduni na Michezo na Mkuu wa wilaya ya Mkuranga, Henry Clemence.

Comments