SIMBA MATAWI YA JUU, YANGA WAIPINDUA AZAM

SIMBA SC jana ilizidi kujinafasi kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, baada ya kuichapa African Lyon mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kwa matokeo hayo Simba imefikisha pointi 50, baada ya kucheza mechi 22, wakati Yanga iliyowafunga wenyeji Coastal Union Uwanja wa Mkwakwani, Tanga jana imefikisha pointi 46 baada ya kucheza mechi 21.
Azam imeshuka hadi nafasi ya tatu kwa pointi zake 44, baada ya kucheza mechi 21, ingawa jana haikuwa dimbani.
Katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ushindi wa Simba ulitokana na mabao ya Salum Machaku dakika ya 33 na Haruna Moshi ‘Boban’ dakika ya 44.
Uwanja wa Mkwakwani Tanga, Yanga ililazimika kusubiri hadi dakika ya 85 kushangilia bao la ushindi, mfungaji mwanasoka Bora wa Uganda 2011, Hamisi Kiiza ‘Diego’.

Comments