Kocha Charles Boniface Mkwasa wa Twiga Stars amemuongeza
mshambuliaji Rehema Salum wa Shule ya Sekondari Lord Baden ya mkoani Pwani
kwenye kikosi hicho kitakachoingia kambini Machi 25 mwaka huu.
Rehema aliibuka mfungaji bora kwenye mashindano maalumu ya
Siku ya Wanawake Duniani yaliyoshirikisha shule nane za sekondari za Mkoa wa Dar es Salaam na kuhitimishwa
Machi 8 mwaka huu.
Twiga Stars itaingia kambini kwenye kambi ya Jeshi la
Kujenga Taifa (JKT) iliyoko Ruvu mkoani Pwani ikiwa ni sehemu ya maandalizi kwa
ajili ya mechi ya mchujo ya Fainali za Wanawake Afrika (AWC) zitakazofanyika
Novemba mwaka huu nchini Equatorial
Guinea .
Timu hiyo itacheza na Ethiopia
kusaka tiketi ya kwenda Equatorial Guinea
ikianzia ugenini Addis Ababa
kwa mechi itakayochezwa Mei 26 mwaka huu. Timu hizo zitarudiana wiki mbili baadaye jijini Dar es Salaam.
Katika
raundi ya kwanza, Twiga Stars iliitoa Namibia kwa jumla ya mabao 7-2. Ilishinda
ugenini 2-0 na kuibuka na ushindi mnono nyumbani wa mabao 5-2.
Machi 10
mwaka huu, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella
Mukangara alizindua akaunti ya Twiga Stars kupitia Tigo Pesa kuichangia timu
hiyo ili ishiriki vyema michuano ya AWC.
Wachangiaji
wa Twiga Stars wanatakiwa kutuma mchango wao kwenda namba 13389 ambapo kiwango
cha juu kinachoweza kutumwa kwa muhamala (transaction) mmoja ni sh. 500,000. Katika
uzinduzi huo, Waziri Dk. Mukangara alichangia sh. milioni moja.
Comments
Post a Comment