JOTO LA BONGO LAICHANGANYA ES SETIF


HALI ya hewa ya joto inaonekana kuwahenyesha wachezaji wa timu ya Es Setiff ya Algeria, ambapo jana walilazimika kuvua jezi na kuyafakamia maji kila wakati, pale walipokuwa wakifanya mazoezi kwenye uwanja wa TFF Karume jijini Dar es Salaam.
Ingawa Kocha Geiger Alain na nahodha wake Slimane Raho, mlinzi mwenye umri wa miaka 36, walisema kuwa hali ya hewa ya joto haitawafanya kupoteza mchezo wa kwanza wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Simba hapo Jumapili, lakini ni dhahiri kuwa joto limewapa wakatimgumu.
Kila mara wachezaji hao walikuwa wakipigana vikumbo kuyafakamia maji ya kunywa ambapo mbali ya kunywa walikuwa wakijimwagia vichwani, katika kile kinachoonekana kuzidiwa na joto.
Ukiondoa tatizo hilo la joto, lakini maumbile makubwa na uwezo wa wachezaji hao vimewatisha mashabiki waliofika kwenye uwanja wa Karume kushuhudia mazoezi yao.
Hii ni kutokana na kwamba asilimia kubwa ya wachezaji hao wana miili mikubwa na mwenye mwili mdogo kwao ndiye unayeweza kumfananisha na wachezaji wetu tunaoweza kuwahesabu kwamba wana miili ya wastani.
“La kama miili ndiyo inayocheza basi Simba wameshafungwa, hawa jamaa wote wana maumbo makubwa ya kimpira rafiki yangu, halafu wanaweza kumiliki mpira na kuuchezea watakavyo, kwa kweli mimi sio mtabiri lakini Simba inabidi wajipange,” alisema shabiki mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Idd Mussa mkazi wa Ilala.

Comments