SHEHATA AIKATA MAINI YANGA


KLABU ya Zamalek, imetupilia mbali ombi la timu ya Yanga ya Tanzania, kutaka kusiwepo mechi ya marudiano baina yao iliyopangwa kupigwa mjini hapa kati ya Machi 2 hadi 4, wakihofia hali ya usalama.
Kwa mujibu wa ratiba ya Shirikisho la Soka Afrika (Caf), mechi hiyo ya marudiano ya hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, itapigwa wiki mbili baada ya ile ya kwanza itakayochezwa Februari 18, kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Awali, uongozi wa Yanga uliandika barua Caf, kupitia Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kuomba uwepo wa mechi moja tu ya kuamua timu ya kusonga mbele katika michuano hiyo, hivyo kufuta mechi hiyo ya marudiano.
Jumanne wiki hii, TFF lilituma ombi hilo Caf, ikitambua kuwa, uamuzi wa jambo hilo ungetegemea matakwa ya Zamalek, iwe kuchezwa mechi moja au pambano hilo kuhamishiwa nchi nyingine kwa sababu za kiusalama.
Yanga, wametaka mechi moja, wakisita kwenda Cairo, Misri kwa mechi ya marudiano, baada ya kutokea vurugu za mashabiki katika mechi ya Ligi Kuu kati ya Ahly na El Masry iliyopigwa kwenye Uwanja wa Port Said.
Katika mechi hiyo, ambayo iliisha kwa Ahly kufungwa mabao 3-1, mashabiki wa El Masry, walivamia uwanja na kuanza kushangilia wakirusha fataki na chupa za maji dhidi ya mashabiki wa Ahly, ambao nao walijibu mapigo.
Hali hiyo ikazusha mapigano na mkanyagano mkubwa hadi kusababisha vifo vya mashabiki takriban 74 na wengine 1,600 kujeruhiwa, hivyo nchi hiyo kuingia kwenye maombolezo ya siku tatu.
Kwa mujibu wa Kocha Msaidizi wa Zamalek, Ismail Youssef, bosi wake (Hassan Shehata), amekataa kucheza mechi moja na kama vipi, wapo tayari mechi hiyo ipigwe bila mashabiki mjini hapa.
“Kocha (Hassan) Shehata amesisitiza kuwa, mechi ya marudiano dhidi ya Yanga, lazima ichezwe Misri, hata kama itakuwa bila mashabiki kwa sababu za kiusalama,”  alisema kocha huyo msaidizi kupitia mtandao.
Zamalek, ambayo mwaka jana iliamriwa kucheza mechi mbili za nyumbani bila mashabiki, kutokana na vurugu za mashabiki wake.
Zamalek wametoa msimamo huo, huku Caf ikitarajia kujadili vurugu hizo kesho Jumamosi, kuangalia hatua za kuchukua dhidi ya waliohusika kwa namna moja au nyingine na maafa hayo makubwa zaidi katika soka ya Misri. 

Comments