OKWI AIPAISHA SIMBA KILELENI


Simba SC wamerejea kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya kuilaza Azam FC mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Shukrani kwake, mshambuliaji wa kimataifa wa Uganda, Emmanuel Arnold Okwi aliyefunga mabao yote hayo, moja kila kipindi akifikisha jumla ya mabao tisa, akiwasogelea John Bocco wa Azam anayeongoza kwa mabao yake 12 akifuatiwa na Kenneth Asamoah wa Yanga, mwenye mabao 10.
Simba imefikisha pointi 37 na kuwaacha kwa pointi tatu, mabingwa watetezi, Yanga ambao leo watakuwa na nafasi ya kuwakamata Wekundu hao wa Msimbazi watakapokuwa wakimenyana na Ruvu Shooting. Simba imecheza mechi moja zaidi ya Yanga.
Katika mechi nyingine za Ligi Kuu jana, Coastal Union ilitumia vizuri Uwanja wake wa Mkwakwani, Tanga kwa kuifunga African Lyon 1-0 bao pekee la Ali Ahmad Shiboli dakika ya 30.
Villa Squad iliwafunga wenyeji Polisi Dodoma mabao 2-1,
kwenye Uwanja wa Jamhuri, Dodoma. Mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Nsa Job jana
alitimzia mabao manne ndani ya mechi tatu kutokana na kufunga mabao yote mawili, dakika ya 20 na 85, wakati la Polisi lilifungwa na Bantu Admin dakika ya 80.
Katika mchezo mwingine, bao pekee la mkongwe Mohamed Simba Banka ‘Figo’ jana liliipa JKT Ruvu ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji JKT Oljoro, Uwanja wa Sheikh Anmri Abeid, Arusha.
Toto African ililazimishwa sare ya bila kufungana na Moro United kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.

Comments

Post a Comment