MJUMBE KAMATI YA UTENDAJI TFF AFARIKI DUNIA

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha aliyewahi kuwa mjumbe wake wa Kamati ya Utendaji, Kassim Kashulwe kilichotokea Februari 9 mwaka huu nyumbani kwake Kigurunyembe mkoani Morogoro.
Licha ya kuwa mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF (wakati huo Chama cha Mpira wa Miguu Tanzania- FAT), pia Kashulwe aliwahi kuwa kiongozi wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Morogoro (MRFA) na baadaye kamishna wa mechi za Ligi Kuu.
Kwa mujibu wa taarifa tulizopata leo (Februari 13 mwaka huu) kutoka MRFA, Kashulwe alifia nyumbani kwake na kuzikwa juzi (Februari 11 mwaka huu) kwenye makaburi ya Kora yaliyoko nje kidogo ya mji wa Morogoro.
Mbali ya Kashulwe, wengine waliochaguliwa katika uchaguzi wa FAT uliofanyika mwaka 1993 mjini Kibaha ni Muhidin Ndolanga (Mwenyekiti), Alhaji Omari Juma (Makamu Mwenyekiti) na Kanali Ali Hassan Mwanakatwe (Katibu Mkuu) na wajumbe Abdul Msimbazi, Amin Bakhresa, Job Asunga, Joel Bendera, Masalu Ngofilo na Wilson Mwanja.
Msiba huo ni pigo kwa familia ya Kashulwe, TFF na familia ya mpira wa miguu nchini kwa kuwa mchango wake ulikuwa bado unahitajika. TFF inatoa pole kwa familia ya marehemu Kashulwe, na MRFA na kuwataka kuwa na uvumilivu kipindi hiki cha msiba huo mzito.
Pia TFF itatoa ubani wa sh. 200,000 kwa familia ya marehemu kama rambirambi zake. Mungu aiweke roho ya marehemu Kashulwe mahali pema peponi. Amina
Boniface Wambura, Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Comments