NI REAL MADRID NA BARCA LEO


Real Madrid inahitaji Cristiano Ronaldo kurejesha kujiamini kwake dhidi ya Barcelona, wakati timu hizo zitakapomenyana kwenye “clasico”, mechi ya kwanza ya Kombe la Mfalme hatua ya Robo Fainali leo.

Ronaldo amefunga mara mbili tu katika mechi 13 dhidi ya Barcelona, bao lake la mwisho akifunga Aprili kwenye fainali ya michuano hiyo na kuipa Madrid ushindi wa kwanza ndani ya mechi 12 dhidi ya klabu hiyo ya Catalan.

Mshambuliaji huyo wa Kireno amekuwa katika wakati mgumu tangu apoteze nafasi kibao za kufunga mabao, siku Madrid ikipigwa 3-1 katika mechi ya Ligi Kuu mwezi uliopita na mwaka huu amefunga bao moja tu hadi sasa.

Ronaldo ndiye anayeongoza kwa mabao yake 21 katika mbio za kiatu cha dhahabu cha La Liga na alipagawa mno Jumamosi, wakati Madrid iliposota kuibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Mallorca na kuiacha kwa pointi tano Barcelona kileleni.

Wakati huo huo, mpinzani wake mkuu wa Barcelona aliyetwaa tuzo ya tatu ya Mwanasoka Bora wa Dunia hivi karibuni, Lionel Messi, aling’ara kwa kufunga mabao mawili akiwawezesha mabingwa hao wa Hispania kushinda 4-2 dhidi ya Real Betis.

Mabao hayo mawili yalimfanya atimize mabao 33 msimu huu— sita zaidi ya Ronaldo.

“Leo wakati wote amekuwa mchezaji ambaye anaweza kufanya mabadiliko, mchezaji wa maana. Na ni mchezaji anayeendana na aina zote za mchezo, ambaye anapenda kucheza,” alisema kiungo wa Barcelona, Xavi Hernandez.

Wakati Ronaldo anatarajiwa kuanza, kocha Jose Mourinho lazima abadilishe mfumo wa uchezaji ambao utamuwezesha kuwasimamisha mabingwa mara 25 wa Kombe hilo, akiwakosa beki Alvaro Arbeloa na kiungo majeruhi Sami Khedira.

Mshambuliaji Angel di Maria alifanya mazoezi kwa mara ya kwanza juzi, lakini Pepe hakufanya, ambayo inamuweka katika wakati mgumu Mourinho, kwa sababu Mreno huyo amekuwa tegemeo la timu hivi karibuni, hususan katika mechi za clasicos.

“Huwezi kucheza vizuri kila mechi,” alisema mshambuliaji wa Madrid, Jose Callejon, baada ya kufunga bao la ushindi dhidi ya Mallorca.

Barcelona itamkosa mshambuliaji wake majeruhi, David Villa na Pedro Hernandez na kiungo Seydou Keita kwenye Uwanja wa Bernabeu, ambao mabingwa hao wa Ulaya hawajafungwa katika mechi sita.

“Tutakwenda huko ili kutafuta nafasi za kufunga mabao na kujaribu pia kucheza soka nzuri kadiri itakavyowezekana,” alisema Pep Guardiola.

Wapinzani hao wa jadi wa Hispania wamegawana mataji 16 ya michuano hiyo tangu mwaka 1916 na kila timu ikishinda nane.

Mshindi wa mechi hii atacheza ama na Valencia au Levante, ambao watamenyana kwenye Uwanja wa Mestalla kesho.

Comments

Post a Comment