Ivory Coast ilifanikiwa kuishinda Burkina Faso 2-0 katika uwanja wa Malabo na kufuzu kuingia robo fainali ya michuano ya Kombe la Mataifa barani Afrika.
Lakini licha ya wachezaji wengi wa Ivory Coast ambao huwa wanacheza katika ligi kuu ya Premier nchini England kuwa uwanjanji, hawakuonyesha mchezo wa kusisimua, kwani wachezaji wa Burkina Faso waliweza kuumiliki mpira kwa muda mrefu.
Kwa kushindwa katika mechi mbili mfululizo, juhudi za Burkina Faso hazikufika popote, na itabidi kurudi nyumbani.Katika mechi iliyotangulia Alhamisi, Sudan iliweza kupata pointi yake ya kwanza katika mashindano hayo, baada ya miaka 36, kufuatia sare ya 2-2 ilipocheza na Angola.
Mechi hiyo pia ilichezewa mjini Malabo.
Manucho alifunga tena kwa mkwaju wa penalti, lakini naye Bashir akapata bao la kusawazisha, katika dakika za mwishomwisho za mchezo.
Mechi za Ijumaa zitachezewa katika uwanja wa Libreville, wakati Gabon, ambao wanashirikiana na Equatorial Guinea kuandaa mashindano, watawakaribisha Morocco.
Hii inatarajiwa kuwa mechi ngumu na ya kusisimua.
Hata hivyo, kabla ya mechi hiyo, Niger, ambayo inashiriki katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa mara ya kwanza, itapambana na Tunisia.
Comments
Post a Comment