TWANGA PEPETA WAREJEA NYUMBANI

Mwandishi wetu

BENDI ya muziki wa dansi ya African Stars “Twanga Pepeta International imewasili leo  kutoka, London, Uingereza na kuweka mikakati yake ya kuhimarisha soko la kimataifa na la hapa nyumbani.

Kauli hiyo ilitolewa na kiongozi wa bendi hiyo, Luizer Mbutu alipokuwa anazungumzia mafanikio na changamoto za maonyesho yao yaliyofanyika nchini Uingereza.

Luizer alisema kuwa wamepata mafanikio makubwa katika maonyesho hayo ya wiki mbili huku moja likiwa la kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania.

Alisema kuwa tofauti na ziara yao ya kwanza ya mwaka 2005, safari hii walikwenda kufanya shoo huku wakizinadi CD na DVD za albamu zao za nyuma zikiwa katika maonyesho ya ‘live’ nay a kawaida ambazo walifanikiwa kuziuza zote.

“Kwa kweli tumefarijika sana na maonyesho na kufanikiwa kuuza kazi zetu nchini Uingereza, kazi iliyobakia sasa ni kuhimarisha soko hilo huku tukifanya kazi kama hiyo hiyo hapa nyumbani,” alisema Luizer.

Alisema kuwa maonyesho yao yalijaza watu mbali mbali wa mataifa tofauti na kupata mwaliko mwingine ambao uongozi utaamua lini watarejea huko.

“Napongeza uongozi wa ASET chini ya Mwenyekiti, Msiilwa Baraka na Mkurugenzi, Asha Baraka kwa kufanikisha ziara hii ya tatu kwa bendi kufanya maonyesho Ulaya, mwaka 2005 tuliweza kufanya maonyesho katika nchi tano za Scandinavia na mwaka uliofuata tukaingia London kwa mara ya kwanza,” alisema.

Alisema kuwa hawakuwa wanakaa tu kusubiri kazi za kufanya maonyesho kwani wameweza kutunga nyimbo mbili, mmoja unajulikana kwa jina la Back to London uliotungwa na Chalz Baba na Uzuri wa Mwanamke mke siyo Tabia bali ulivyopendezewa uliotungwa na Saleh Kupaza.
Alisema kuwa nyimbo hizo zitafanyiwa mazoezi ili kuzihimarisha na kuanza kupigwa katika maonyesho yao mbali mbali ya mwisho wa wiki hii.

Mkurugenzi wa bendi hiyo, Asha Baraka aliwapongeza wote waliofanikisha ziara hiyo na kusema kwa ssa wanajipanga kwa ajili ya maonyesho ya hapa nyumbani na ziara nyingine za nje ya nchi.

Comments