TASWA YAMTEUA DAMAS NDUMBARO KUSIMAMIA MAREKEBISHO YA KATIBA


(TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI)

(A) MAREKEBISHO YA KATIBA

KAMATI ya Utendaji ya Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), ilikutana hivi karibuni pamoja na mambo mengine ilikubaliana kufanya marekebisho madogo ya Katiba ya chama hicho ili iendane na wakati wa sasa.

Kutokana na hali hiyo Kamati ya Utendaji inemteua mwanamichezo maarufu ambaye pia ni mwanasheria na wakala wa wachezaji wa soka Damas Ndumbaro kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Marekebisho  ya Katiba ya TASWA.

Wajumbe wengine kwenye kamati hiyo ni George John ambaye ni Katibu Mkuu Msaidizi wa TASWA,Alfred Lucas ambaye ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TASWA na Amir Mhando ambaye ni Katibu Mkuu wa TASWA na atakuwa Katibu wa kamati hiyo na Mwani Nyangasa ambaye ni mwanachama.

Kamati hiyo itasimamia mchakato wa marekebisho hayo, kisha utaitishwa Mkutano Mkuu Maalum wa wanachama wote kwa ajili ya kupitia rasimu hiyo na ni imani ya Kamati ya Utendaji kuwa marekebisho hayo ya Katiba hayatachukua muda mrefu, ili mkutano Mkuu wa TASWA ufanyike kabla ya kumalizika robo ya kwanza ya mwaka 2012.

(B) SEMINA, MAFUNZO MWAKA 2012
Kikao hicho pia kilipanga kuhusiana na masuala mbalimbali ya mafunzo kwa wanachama wake mwaka 2012, ambapo Sekretarieti ya TASWA imepewa jukumu la kuratibu tarehe ya mafunzo yote na italitolea taarifa kwa vyombo vya habari Jumapili Januari mosi, 2012 kwa kuanzia na mafunzo ya Kanda ya Kaskazini, ambayo awali ilikuwa yafanyike Novemba mwaka huu.

(C) MSIBA WA WANAHABARI
TASWA inatoa pole kutokana na misiba ya wanahabari ambao pia ni wanamichezo Halima Mchuka aliyefariki dunia jana na John Ngahyoma aliyefariki dunia leo.

TASWA imeshtushwa taarifa za vifo hivyo na inatoa pole kwa familia za wafiwa, wanahabari na  wanamichezo wengine katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na wapendwa wetu. Mungu aziweke mahali pema peponi roho za wafiwa. Amin

Comments