CHAMA cha Mpira wa Miguu Uingereza (FA) kimetuma maombi
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kumuombea Hati ya Uhamisho wa
Kimataifa (ITC) mchezaji Douglas Didas Masaburi ili ajiunge na klabu ya nchini
humo. Masaburi mwenye umri wa miaka 21 anaombewa ITC ili ajiunge
na klabu ya Coventry Spartans akiwa mchezaji wa ridhaa. Coventry Spartans iko
katika Ligi Daraja la Pili ya Midland. Mchezaji huyo anaombewa ITC kutoka katika klabu ya New Rule
Power. TFF inafanyia kazi maombi hayo na hati hiyo itatolewa mara baada ya
taratibu husika kukamilika. Aidha, Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi
kutoka Zambia kuchezesha mechi ya kwanza ya mchujo ya Kombe la Afrika kwa
Wanawake (AWC) kati ya Tanzania (Twiga Stars) na Namibia. Mechi ya kwanza itachezwa jijini Windhoek, Namibia kati ya
Januari 13, 14 na 15 mwakani. Mwamuzi ni Gladys Lengwe wakati waamuzi wasaidizi
ni Patience Mumba na Mercy Zulu. Mwamuzi wa akiba (mezani) atakuwa Bookanang Lekgowe kutoka
Botswana wakati kamishna wa mechi hiyo kutoka Afrika Kusini atakuwa Smith
Hilton Fran. Mechi ya marudiano itachezwa Januari 29 mwakani Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam. Twiga Stars inayofundishwa na kocha Charles Boniface
Mkwasa akisaidiwa na Nasra Mohamed imeanza rasmi mazoezi jana (Desemba 19 mwaka
huu) kwa ajili ya mechi hiyo. Katika hatua nyingine, Watanzania wawili, Leslie Liunda na Joan Minja wamechaguliwa kuwa
wakufunzi wa waamuzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) baada ya
kufaulu katika kozi iliyofanyika Mei mwaka jana jijini Cairo, Misri. Minja ambaye pia ni Katibu wa Kamati ya Waamuzi ya
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Liunda ni miongoni mwa zaidi ya
waamuzi wa zamani 90 walioshiriki kozi hiyo ambapo jumla ya waliofaulu na
kupata ukufunzi wa CAF ni 58 wakiwemo wanawake tisa. Ukanda wa CECAFA (Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika
Mashariki na Kati) umetoa jumla ya wakufunzi tisa kutokana na kozi hiyo.
Wakufunzi hao kwa upande wa wanawake ni Minja (Tanzania), Gladys Waweru (Kenya)
na Catherine Adipo (Uganda). Kwa upande wa wanaume ni Liunda (Tanzania), Ali Waiswa
(Uganda), Bernard Mfubusa (Burundi), Eshetu Sheferaw (Ethiopia), Jumaa Kaluwe
(Kenya) na Salih Mohamed (Sudan). Watanzania wengine ambao waliwahi kuwa wakufunzi wa waamuzi
wa CAF ni Gratian Matovu, Joseph Mapunda na Alfred Lwiza.
Comments
Post a Comment