NGUMI KUPIGWA DDC KEKO DESEMBA 9

BONDIA wa ngumi za kulipwa nchini, Ramadhan Nassib, anatarajia kupanda ulingoni kuzichapa na mpinzani wake Antony Kariuki wa Kenya, katika pambano la maadhimisho ya miaka 50 ya Uhuru litakalopigwa kwenye Ukumbi wa DDC Keko Dar es Salaam, Desemba 9 mwaka huu.

Akizungumza Mratibu wa pambano hilo, Pius Aghaton, alisema kuwa pambano hilo linatarajiwa kuwa na upinzani mkali kutokana na rekodi zilizopo kwa mabondia wote.
Alisema kuwa pambano hilo litakuwa la uzito wa Fly ambalo litapigwa katika raundi 10.
“Tumeandaa pambano la aina yake kwa ajili ya kusherekea miaka 50 ya Uhuru na pia kuweza kuwajengea mabondia wetu uwezo wa kucheza mapambano ya kimataifa” alisema.
Mratibu huyo alisema kuwa katika pambano hilo, kutakuwa na mapambano ya utangulizi ambapo bondia Juma Fundi atazichapa na Juma Seleman katika pambano la uzito wa Fly la raundi sita, Fred Sayuni atazipiga na Bakari Dunda katika pambano la uzito wa Feather la rfaundi sita.
Pambano jingine litawakutanisha mabondia Rashid Ally pamoja na Daud Mhunzi katika pambano la uzito wa Feather la raundi sita na Faraji Sayuni atazichapa na Alpha George katika pambano la uzito wa Fly la raundi nne.
Katika Mchezo huo kutakua na DVD za mafunzo ya mchezo wa ngumi pamoja na kutambua sheria zake mbalimbali zitakazokua zikisambazwa na kocha wa mchezo huo Rajabu Mhamila 'Super D Boxing Coach' kwa ajili ya kuwapa mambondia mbalimbali mbinu za mchezo na mashabiki kujua sheria za masumbwi.
Super D alisema katika DVD hizo kutakuwa na mapambano mengi ambayo yanaweza kutumika kama mafunzo muhimu kwa mabondia ,makocha marefa pamoja na mashabiki wa mchezo kujua sheria mbalimbali.

Comments