HATUPO KWA AJILI YA KUIFUNGA YANGA, AKILI ZETU KWENYE UBINGWA TU-SIMBA

Wajumbe wa Kamati ya Utendaji walieleza kusikitishwa kwao na kufungwa na Yanga katika mchezo wa Ligi Kuu msimu huu.
Kamati inafahamu machungu ambayo wapenzi na wanachama wa Simba waliyapata baada ya kipigo hicho.
Hata hivyo, Kamati inasisisitiza kuwa ni vema wapenzi wa Simba wakaanza kuitazama ligi kwa mapana yake. Ligi haipo kwa ajili ya Simba kuifunga Yanga pekee bali kutwaa ubingwa wa Tanzania na kuwakilisha Taifa katika michuano ya kimataifa.
Pamoja na kufungwa na Yanga, Simba inaongoza ligi si kwa kuwa na pointi nyingi pekee bali pia kwa kuwa na idadi kubwa ya magoli ya kufunga na wastani mzuri wa magoli ya kufunga na kufungwa.
Hii ni ishara kuwa Simba ni timu bora Tanzania kwa sasa kwa vigezo vyovyote vile vya kimpira.
Kitendo cha washabiki kutuhumiana, kugombana na kutaka kufanya fujo kwa sababu ya kupoteza mechi moja na kusahau mazuri yote ambayo yamefanywa na timu ni kinyume cha uanamichezo.
Timu kubwa kama Man United ya England zimefungwa hadi mabao sita katika mechi ya watani wa jadi lakini hakuna aliyefanya fujo kwa wachezaji, benchi la ufundi au viongozi wa timu hiyo.
Kamati imehimiza umoja na mshikamano miongoni mwa wana Simba ndani na nje ya nchi. Hakuna sababu ya kuibua migogoro na migongano isiyo na sababu kwa sababu ya timu kupoteza mechi moja.

Naomba kuwasilisha
Ezekiel Kamwaga
Msemaji
Simba Sports Club

Comments

  1. YANGA BOMBA- UHURU BRANCHNovember 8, 2011 at 7:10 PM

    NA NYIE BADO MNAWEWESEKA NA KIPIGO TU!POLENI SANA MTATOA SANA STATEMENT ZA KUHALALISHA KIPIGO LAKINI HAITASAIDIA SANA MPAKA MTUFUNGE NDIO WANACHAMA WATATULIA,NA MSIOMBE TUWATANDIKE TENA...........!

    MDAU WA BOMBA- USA

    ReplyDelete

Post a Comment