NELLY KAMWELU APEWA NAFASI NYINGINE YA KUJARIBU KIMATAIFA

Miss Universe Tanzania 2011 Nelly Kamwelu amepewa nafasi nyingine ya kushindania taji la Miss International lililopangwa kufanyika, Chengdu, China.


Nelly alikuwa mmoja wa warembo walioshindana katika mashindano ya Miss Universe yaliyofanyika nchini Brazil mwezi mmoja uliopita na kushindwa kufanya vyema.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Compass Communication Tanzania Limited, Maria Sarungi Tsehai amesema kuwa Nelly ana vigezo vya kuiwakilisha nchi katika mashindano hayo kutokana na uzoefu alioupata katika mashindano ya Miss Universe.
Maria alisema kuwa Nelly ambaye kwa sasa ni mrembo anayeshikilia taji la Miss Southern Africa alitarajiwa kuondoka jana tayari kuwahi siku ya kwanza ya kambi ya mashindano hayo iliyopangwa kuanza Oktoba 20.
Alisema kuwa kambi hiyo itakuwa ya wiki tatu na mrembo wao amejiandaa ipasavyo ili kufanya vyema. Alisema kuwa ameandaliwa mavazi mbalimbali yenye asili ya kitanzania na baadhi kutoka kwa wabunifu wa hapahapa nyumbani.
“Hii inatokana na ukweli kuwa akiwa huko atashindana katika mavazi mbalimbali ikiwemo vazi la jioni, vazi la taifa ambalo limebuniwa na Diana Magesa na vazi la ufukweni ambalo limebuniwa na Vida Mahimbo,” alisema Maria.
Mbali na mavazi lakini pia watawania tuzo ndogondogo kama vile talent(kipaji), mvuto katika picha (Miss Photogenic) na mahusiano mema(Miss Congeniality).

Comments